Mara nyingi watu hawapendi kujioa wao peke yao.

Sisi binadamu ni viumbe wa kujumuika, na moja ya lengo letu kubwa kwenye maisha ni kuhakikisha hatupo peke yetu, kuna watu ambao wako sawa na sisi na tupo pamoja nao.

Turudi nyuma kidogo wakati tupo watoto na tunasoma shule za msingi. Idadi ya marafiki uliokuwa nao ilikuwa kigezo muhimu sana cha kupima mafanikio yako ya kijamii kwa wakati huo. Hivyo wengi tulilazimika kujihusisha na vikundi fulani vya kirafiki, hata kama vilikuwa haviendani na sisi.

Inatisha sana kuwa uko peke yako, na kwa sababu hatupati elimu ya kujielewa kwamba hata tunapokuwa wenyewe bado tunaweza kuyafurahia maisha, tumekuwa tunalazimisha kukubalika na vikundi fulani, au kuhakikisha watu wanakubaliana na sisi.

Sasa tunakuja kwa tabia za walioshindwa.

Hawapendi kuwa peke yao, wanahakikisha sio wao tu wameshindwa, kwanza wataonekana ni wazembe.

Hivyo wanahakikisha wanakuwa na kundi la wengine walioshindwa, pamoja na yote kifo cha wengi ni harusi, na hivyo kuwepo na walioshindwa wengi ni faraja kubwa sana.

Wanatimizaje lengo lao hilo? Kwa kuhakikisha kila wanayekutana naye naye anashindwa, na hata kama anajaribu basi watahakikisha wanamfanya wasiweze kwenda mbali zaidi. Watamwambia maneno mengi ya kutisha kuhakikisha anaachana na mipango yake na kujiunga na kundi lao, kundi la walioshindwa.

Ufanye nini kuepuka hili kwneye maisha yako?

Kwanza kabisa wamulike watu wote wanaokuzunguka, marafik, ndugu, jamaa, wafanyakazi wenza, wafanyabiashara wenzako na kila mtu mwingine yeyote. Angalia tabia zao je ni watu walioshinda au wanaoelekea kushindwa au ni watu ambao wameshindwa.

Pili tafakari kila aina ya ushauri ambao umekuwa unapokea kutoka kwa watu hao, je umekuwa wa kukupa moyo na kukusukuma au wa kukuvunja moyo na kukurudisha nyuma.

Tatu chukua hatua, kama ni watu walioshindwa na wanakazana kukufanya na wewe ushindwe, wakimbie. Haraka sana.

Na kama wewe ndio mshindwa mwenyewe na umekuwa unawaingiza wengine kwenye kundi lako la washindwa, kwa kuwakatisha tamaa, acha mara moja.

SOMA; WORLD CLASS; Dalili Saba Kwamba Tayari Wewe Una Mtizamo Chanya Utakaokufikisha Kwenye Mafanikio Makubwa.

TAMKO LANGU;

Nimejua ya kwamba walioshindwa wanapenda kuwa na kundi la walioshindwa pia. Mimi nimeamua kuepuka makundi ya aina hii na sitamwingiza mtu yeyote kwenye makundi ya aina hii. Nimechagua maisha ya mafanikio na nitayafanyia kazi kila siku.

NENO LA LEO.

Losers live in the past. Winners learn from the past and enjoy working in the present toward the future.

Denis Waitley

Walioshindwa wanaishi kwenye siku za nyuma. Washindi wanajifunza kutokana na yaliyopita na kufurahia kufanyia kazi sasa ili kuwa na kesho bora.

Epuka mtu yeyote aliyeshindwa, maana atahakikisha na wewe unatumbukia kwenye shimo alilo yeye.

Rafiki na Kocha Wako,

Makirita Amani,

makirita@kisimachamaarifa.co.tz

TUPO PAMOJA.