Sina shaka hakuna ubishi katika hili, kitendo cha kuweka nguvu zako za mawazo katika ndoto yako, ni hatua muhimu sana ya kukusaidia kuweza kutimiza ndoto yako yoyote ile uliojiwekea na hakuna kipingamizi kitakachokuzuia.

Bila ya kuwa na nguvu ya uzingativu, unaona hakuna matokeo makubwa utakayoyapata, na hiyo haitoshi utakuwa hausogei sana katika kile unachokifanya, yaani utakuwa ni kama mtu unajichelewesha kwa sababu ya kukosa nguvu ya uzingativu.

Kwa hiyo, unaweza ukawa una baki na maswali sasa ni kitu kipi kifanyike ili kufanya nguvu zako za uzingativu  zitumike kwa ufasaha na zikupe mafanikio? Je, ni mbinu zipi utumie ili kuongeza uzingativu kwenye ndoto yako hadi kufanikiwa?

2d114-baby-steps-to-success

Hapa katika makala haya, zipo dondoo kadhaa ambazo tumekuandalia zikusaidie katika kuongeza uzingativu kwenye ndoto yako hadi kufanikiwa.

  1. Jenga picha kubwa.

Hakuna muujiza mkubwa utakaokufanya uendelee kubaki kwenye ndoto yako na hadi kukupa mafanikio zaidi ya kujenga picha kubwa ya kile unachokitaka. Jiulize, ni nini unachokitaka? Ni mafanikio yapi unayoyataka? Mafanikio hayo unayoyataka unatakiwa kuyajengea ile  picha unavyotaka yawe.

Kwa mfano, kama unataka kumiliki kampuni kubwa ione kampuni hiyo kwenye akili yako kwanza. Kama unataka kuwa mfanyabiashara mkubwa, tengeneza picha ya mafanikio hayo na kujiona kama unayefaidi matunda hayo. Kujenga picha kubwa kunakusaidia kukuongezea uzingativu na mwisho wa siku unatimiza ndoto yako.

SOMA; Tupa Sababu Zako Kule…Anza Kutimiza Ndogo Zako Hivi.

  1. Jifunze kusema HAPANA.

Kati ya neno ambalo watu wenye uchungu wa maisha yao wanajua kulitumia vizuri ni neno HAPANA. Wanajua vizuri kusema hapana kwa mambo ambayo wanaona wazi kabisa hayawasaidii na yanawapotezea pesa na wakati mwingine na muda pia. Hapa, huwa hawaoni haya kusema hapana bila kuogopa kitu.

Ni rahisi sana kutoka kwenye uzingativu wa ndoto zako kama hujui kusema hapana. Wapo watu watakutaka utumie muda wako kufanya mambo yao, ukikubali utajikuta unapoteza mwelekeo wa ndoto zako. Siri ya kuendelea kubaki kwenye ndoto zako, hebu jifunze kusema hapana karibu kwa kila kitu ambacho hakiendani na ndoto yako.

  1. Kumbuka kila wakati kwa nini ulianza.

Unapoanza jambo lolote, zinakuwepo zipo sababu nzuri sana kwa nini ulianza jambo hilo. Sasa kila wakati unatakiwa uwe unajikumbusha wewe mwenyewe kwa nini ulianza kufanya hicho unachokifanya sasa. Kama ni biashara, kazi au huduma fulani, tafuta muda na jikumbushe kwa nini ulianza?

Kwa kadri jinsi unavyojikumbusha inakusaidia kukupa nguvu  na kukuongezea uzingativu kwenye ndoto yako uliyonayo, hali ambayo itakufanya uzidi kuvuta mafanikio na mwisho wa siku utashangaa zile ndoto zako kubwa zinaweza kufanikiwa kwa jinsi unavyotaka iwe. Amini ndoto zako zitakuwa karibu sana kama kila wakati ukikumbuka kwa nini ulianza.

SOMA; Sifa Nne (4) Za Watu Wasiokata Tamaa.

  1. Panga mipango yako vizuri.

Unatakiwa kupanga mipango yako vizuri kwa kuweka vipaumbele ya nini ufanye na nini usifanye ili ufanikiwe. Unapoweka vipaumbele vyako vya siku, juma na hata mwezi vinakusaidia kukufanya wewe nguvu zako nyingi uelekeze kwenye ndoto zako tofauti na ambapo ungeweza kuishi kiholela na hadi unashindwa kufanikiwa.

Kwa kuhitimisha, najua umejifunza jinsi unavyoweza kuongeza nguvu ya uzingativu hadi kufanikiwa. Ni wajibu wako wewe kufanyia kazi mambo hayo muhimu kwako ili kubadili maisha yako na kuwa ya mafanikio kabisa.

DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,

Ni wako rafiki katika mafanikio,

Imani Ngwangwalu,

Mshauri wa mafanikio, mwandishi na mjasiriamali,

Tovuti; www.amkamtanzania.com

Mawasiliano; +255 767 048 035, +255 713 048 035,

Email; dirayamafanikio@gmail.com