Kitu kimoja ambacho sisi binadamu tunapenda ni uhakika. Tunapenda kufanya kitu ambacho tuna uhakika nacho. Ndiyo maana licha ya kuwepo kwa fursa nyingi na nafasi nyingi za kuchukua hatua, bado watu wengi wanashindwa kujua ni hatua gani wachukue. Kwa sababu hatua nyingi za kuchukua zinakuwa hazina uhakika kama ni sahihi au la.

Kuna wakati tunaweza kuwa tunataka kuchukua hatua fulani, mioyo yetu inatusukuma kabisa kuchukua hatua, lakini akili zinatuambia hatuna uhakika. Hapa wengi hukwama huku wakiwa wamekwazika.

kukosa uhakika

Kitu muhimu kabisa cha kufanya kwenye nyakati kama hizi ni kuchukua hatua hata kama huna uhakika. Kwa kuwa uhakika siyo kitu cha kutegemea kwenye zama hizi, na kwa kuwa mambo yanabadilika, na kwa kuwa chochote kinafaa kuboreshwa zaidi, chukua hatua hata kama huna uhakika.

Kuliko kuacha kuchukua hatua kwa sababu huna uhakika, ni bora kuchukua hatua, halafu kama utakosea utajirekebisha, baada ya kuwa umechukua hatua. Na katika kuchukua kwako hatua utajifunza zaidi kuliko usipochukua hatua.

SOMA; UKURASA WA 1002; Kujua Kila Kitu Na Kujifunza Kila Kitu…

Mambo yote mazuri huwa yanatokea pale mtu anapochukua hatua hata kama hana uhakika kabisa. Kwa sababu wengi nao wanakuwa hawachukui hatua kwa sababu hawana uhakika, hivyo hilo linakuweka mbele, unakuwa mtu pekee unayechukua hatua.

Pia unapochukua hatua bila ya uhakika, inakufanya uwe mwangalifu, uwe tayari kujifunza na kuepuka kufanya kwa mazoea, hayo yote yanaongeza ufanisi kwenye ufanyaji wako.

Usisubiri mpaka upate uhakika, dunia ya sasa kitu uhakika kilishapotea kabisa, wewe fanya, fanya kile ambacho ni sahihi, na utaona njia sahihi zaidi kadiri unavyokwenda.

Kila la Kheri Rafiki Yangu.

Rafiki na Kocha wako,

Makirita Amani,

Kwa kupata vitabu vya biashara na mafanikio tembelea www.kisimachamaarifa.co.tz/vitabu

Kupata blog ya kitaalamu unayoweza kuitumia kutengeneza kipato tembelea www.mtaalamu.net/patablog