“We can understand wisdom in three ways: first, by meditation; this is the most noble way. Secondly, by being influenced by someone or following someone; this is the easiest way. Third is the way of experience; this is the most difficult way.” —CONFUCIUS

Unaweza kupata hekima kwa njia kuu tatu,
Njia ya kwanza ni kupitia tahajudi, hii ndiyo njia bora kwa kuwa inaipa akili yako nafasi ya kuweza kuona kile ambacho tayari kipo. Kwa kukosa utulivu na umakini na kusumbuliwa na kelele nyingi, akili yako inashindwa kuona vitu ambavyo viko wazi kabisa.
Hivyo kupitia tahajudi, unatuliza akili yako na kupata umakini mkubwa na hivyo kuweza kupata hekima.

Njia ya pili ni kupitia ushawishi wa wengine, hapa unajifunza kupitia wale wenye hekima.
Unaweza kujifunza kupitia kusoma vitabu vilivyoandikwa na wenye hekima au kuwafuatilia wale wenye hekima na kujifunza kupitia maisha yao.
Njia hii ni rahisi, kufuatilia au kujifunza kwa wengine hakuhitaji nguvu kubwa.

Njia ya tatu ni uzoefu binafsi, kupitia yale unayofanya na matokeo unayopata.
Unapochukua hatua fulani na ukakosea au kuumia, unajifunza kwamba hizo siyo hatua sahihi kuchukua.
Unapochukua hatua nyingine na ukafanikiwa, unajifunza kwamba hizo ndiyo hatua sahihi kuchukua.
Njia hii ni ngumu kwa sababu utachukua muda mrefu sana kujifunza kwa uzoefu kitu ambacho ungeweza kujifunza kwa muda mfupi kipitia wengine.

Ili kupata hekima zaidi kila wakati, tumia njia zote tatu.
Fanya tahajudi mara kwa mara kwa lengo la kutuliza akili yako na kuongeza umakini ili uweze kufikiri na kufanya maamuzi sahihi.
Jifunze kupitia wengine, kwa jinsi wanavyofanya mambo yao na kwa vitabu walivyoandika. Angalia makosa waliyofanya na usirudie, angalia mazuri waliyofanya na yarudie.
Jifunze kupitia hatua unazochukua, kwa kila unalofanya, mwisho fanya tathmini, umefanya vizuri kiasi gani, wapi pa kuboresha, kipi cha kufanya zaidi na kipi cha kuacha kufanya.

Tumia njia hizo tatu kila wakati na utaweza kujijengea hekima kubwa.
#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
Wako rafiki katika safari ya kuelekea kwenye mafanikio makubwa,
Kocha Dr Makirita Amani,
http://www.t.me/somavitabutanzania