Rafiki yangu mpendwa, leo tunakwenda kuuongelea uhuru kwa mapana yake, kwa namna ambayo hujawahi kuuangalia ili wewe mwenyewe uone ni jinsi gani umekuwa unachagua kupoteza uhuru wako.
Kuna mambo unafanya, ambayo unaona ni ya kawaida kabisa lakini ndiyo yanakunyima uhuru wako. Kabla hatujaingia kwa kina kuona jinsi unapoteza uhuru wako, tupate nukuu kutoka kwa Bill Cunningham, aliyekuwa mpiga picha maarufu. Nukuu zake zinaeleza vizuri kile ambacho tunakwenda kujifunza leo.
“If they pay you, they get to tell you what to do. If you don’t take money, they can’t tell you what to do, kid.” – Bill Cunningham
Akimaanisha; wakishakulipa wanakupangia nini cha kufanya. Usipochukua fedha zao, hawawezi kukupangia ufanye nini.
“Money’s the cheapest thing. Liberty, freedom is the most expensive.” – Bill Cunningham
Akimaanisha fedha ndiyo kitu cha bei rahisi zaidi, uhuru ndiyo kitu cha bei ghali zaidi.
Ukishalipwa huna tena uhuru.
Sikuwahi kuielewa nguvu iliyo nyuma ya kumlipa mtu mpaka nilipoanza kuwalipa watu kwa kazi mbalimbali.
Mara kwa mara nimekuwa naona hili, mtu ambaye unampa kazi fulani ya kufanya, yeye ndiyo mtaalamu wa kazi hiyo. Unajaribu kumpa mapendekezo yako, ukitegemea yeye atafanya kwa ubora akizingatia utaalamu na uzoefu wake. Lakini mwisho wa siku kinachotokea ni anafanya kama ambavyo wewe unataka, hata kama haiendani na kile anachojua yeye ni bora.
Ukweli ni kwamba, mtu akishakulipa, anakuwa kama amekumiliki, anaweza kukupangia ufanye nini hata kama kwako hakina maana yoyote.
Na hasa pale unapokuwa na uhitaji mkubwa wa fedha, pale ambapo huwezi kusema hapana kwenye fedha, basi ndiyo uhuru wako unapotea kabisa. Utajikuta unafanya vitu ambavyo wewe mwenyewe unajua havina maana, ambavyo ingekuwa ni maamuzi yako usingefanya, lakini kwa kuwa umeshalipwa au unategemea kulipwa basi unafanya.
Utaishije bila kulipwa?
Hili ndiyo swali ambalo unajiuliza, kwamba utaishije bila ya kulipwa, unahitaji fedha ya kuendesha maisha yako, na fedha hiyo inabidi uipate kwa wengine. Sasa hapo unaipataje?
Hapa nina majibu mawili kwako, ya jinsi ya kupata uhuru wako huku ukiendelea kulipwa na wengine.
Moja; usitegemee malipo ya mtu mmoja.
Kama unategemea mtu mmoja akulipe, basi jua mtu huyo anakumiliki. Hakuna lugha nzuri zaidi ya hiyo, kwa maneno mengine tunaweza kusema wewe ni mtumwa wa mtu huyo. Kwa sababu akiamua kuacha kukulipa leo, maisha yako yatakuwa kwenye hali mbaya sana. Hivyo hata kama hatakuambia, wewe utajiongeza mwenyewe, kwa kumnyenyekea ili kuhakikisha anaendelea kukulipa.
Hakikisha kipato chako kinatoka kwenye vyanzo vingi na watu wengi, kiasi kwamba unakuwa na uhuru wa kuchagua ufanye kazi na nani na nani usifanye naye kazi.
Kwa mfano kama una biashara, una uhuru wa kuchagua uhudumie wateja wa aina gani, wateja ambao wanaheshimu thamani unayotoa na unaweza kwenda nao. Na wale ambao hawaheshimu unachofanya na kufikiri wanaweza kukupelekesha kwa sababu wanakulipa, una nguvu ya kuwaambia hutaendelea kufanya nao biashara. Hapa unakuwa na nguvu na uhuru mkubwa wa kufanya mambo yako.
Ndiyo maana nimekuwa nakusisitiza sana, kama umeajiriwa, kuwa na biashara ya pembeni, na kwenye kitabu cha BIASHARA NDANI YA AJIRA nimekupa mbinu zote za kuweza kuanzisha na kukuza biashara yako ukiwa kwenye ajira. Kupata kitabu hiki cha BIASHARA NDANI YA AJIRA, piga simu 0678 977 007. Ukiweza kuanzisha biashara ukiwa kwenye ajira na ikakuingizia kipato, unakuwa huru zaidi kuliko unapokuwa unategemea mshahara pekee.
Mbili; kuwa na fedha za kukutosha kumtukana bosi wako.
Kuna kauli ya Kiingereza inaitwa “f*ck you money” hiki ni kiwango cha fedha ambacho ukiwa nacho unaweza kumtukana yeyote anayekupangia cha kufanya bila ya kujali atafanya nini.
Hapa unakuwa umejijengea uhuru wa kifedha, kwa kuwa na akiba na uwekezaji wa kutosha kukupa kipato cha kuendesha maisha yako hata kama hufanyi kazi moja kwa moja.
Unafanya kazi kwa sababu ni kitu unachopenda kufanya, na hivyo mtu anapokulazimisha ufanye kile ambacho hakina maana kwako, uko tayari kuwaambia hutaki kufanya na wafanye chochote wanachotaka.
Ili kufikia ngazi hii lazima uwe mzuri sana kwenye kazi unayofanya, na pia lazima uwe umejijengea msingi mzuri kifedha. Kufikia kiwango hiki, unahitaji sana mafunzo yanayopatikana kwenye kitabu cha ELIMU YA MSINGI YA FEDHA, ambacho kinakupa mafunzo ya kuongeza kipato chako, kuweka akiba na kuwekeza ili uwe na uhuru wa kifedha. Kukipata kitabu piga simu 0678 977 007.
Fedha ni rahisi, uhuru ni ghali.
Rafiki, kama tumekwenda sawa mpaka sasa, umejionea mwenyewe kwamba kitu muhimu zaidi kwenye maisha yako siyo fedha bali uhuru. Kwa sababu siyo ngumu kupata fedha, kama ukiwa tayari kutumikishwa au kupelekeshwa na yeyote, utapata tu fedha.
Na hili tumekuwa tunaliona kila siku, watu wenye uwezo mkubwa wakikubali kuwa watumwa wa watu wasio na uwezo wowote, ila tu wana fedha za kuwalipa, wakati mwingine hata hizo fedha siyo zao.
Tumekuwa tunaona wanasiasa ambao hawana ujuzi wowote kwenye eneo fulani, wakitoa maagizo ambayo wenye ujuzi wanalazimika kuyafuata, kwa sababu tu wanasiasa hao wana nguvu ya kuathiri kipato chao.
Kitu muhimu unachopaswa kupambana nacho kwenye maisha yako ni uhuru kwanza, na unapaswa kuanza na uhuru wa kifedha, ili uweze kuwa na uhuru kamili wa maisha yako.
Weka mpango wako sasa wa kufikia uhuru wa kifedha, jipe miaka ambayo utaendelea kutumika na wengine, lakini ukijenga uhuru wako. Na baada ya hapo, kuwa huru kuyaishi maisha yako.
Usipopanga hivi, utaishia kuwa mtumwa wa wengine maisha yako yote, hawatakuambia kwamba wewe ni mtumwa wao, lakini wewe utajua na wao watajua, kwamba kadiri unavyowategemea wakulipe, ndivyo wanavyoweza kuamua wanakutumiaje.
Karibu tufanye kazi pamoja, ili uweze kujijengea uhuru wa kifedha, ambao utakupa uhuru kamili wa maisha yako. Karibu ujiunge na KISIMA CHA MAARIFA ambapo kuna mafunzo na miongozo ya kukuwezesha wewe kuwa huru na maisha yako. Kujiunga na KISIMA CHA MAARIFA, tuma ujumbe kwa wasap namba 0717 396 253 wenye maneno KISIMA CHA MAARIFA na utapewa maelekezo ya kujiunga.
Rafiki, kama ungependa kuendelea kupokea makala na mafunzo mengine mazuri kwenye email yako, fungua hapa na ujaze fomu; www.bit.ly/amkaemail
Makala Hii Imeandikwa Na Dr. Makirita Amani Ambaye Ni Daktari Wa Binadamu, Kocha Wa Mafanikio, Mwandishi Na Mjasiriamali.
Kupata vitabu na uchambuzi wa kina wa vitabu jiunge na channel ya SOMA VITABU TANZANIA kwa kufungua kiungo hiki; www.t.me/somavitabutanzania