MAKALA HII IMEANDIKWA NA IMANI NGWANGWALU WA TANGA TANZANIA.

Watu wengi wamefundishwa jinsi ya kuwa na ujuzi kwa ajili ya kuajiriwa na wengine au kujiajiri lakini si kwa ajili ya kupata utajiri na kujitegemea kifedha. Wapo wengine ambao wamejitumbukiza katika kusaka utajiri bila kujua chochote ni namna gani huo utajiri hutafutwa.

Watu hawa hawana kosa hawakupewa siri ya kutengeneza pesa na kujenga utajiri zaidi ya kukaa tu na kusubiri mshahara. Ili kuwa tajiri huna budi kuwa na zana zinazotakiwa katika kuusaka huo utajiri.

Katika makala haya utajifunza kanuni za msingi ambazo unaweza kuzitumia kwa kujijengea uwezo binafsi wa kutengeneza pesa na hatimaye kuwa tajiri. Kanuni hizo ni zipi?

Zifuatazo ni kanuni za msingi zitakazo kuongoza katika njia ya mafanikio na kuwa huru kifedha:-

1. Unapopata kiasi chochote cha pesa weka kidogo kama akiba!

Huna budi kutunza asilimia kumi ya kile unachochuma. Jilipe wewe kwanza. Weka kwenye kisanduku hela hiyo hata kama ni kidogo kwani ndiyo malipo yako wewe mtafutaji. Hiyo itakuwa akiba yako ya baadae.Utajikuta hela hiyo baada ya miaka mitatu au mitano itakuwa nyingi kiasi cha kwamba itakusaidia kama mtaji kufungua miradi mingine unayotaka kuanzisha.

2. Dhibiti matumizi yako.

Ukiwa na matumizi makubwa na ukiweza kudhibiti matumizi yako, hiyo asilimia kumi ya mapato utaipata. Maana ukiwa na matumizi ya hovyo itapelelekea wewe kupoteza pesa nyingi ambazo zilikuwa hazina sababu ya kupotea, kama unanunua kitu jiulize wewe mwenyewe kwa nini unanunua na kwa sababu gani?

Cha kufanya ili uweze kudhibiti matumizi yako ni lazima ujue vyanzo vya fedha zako ni nini? Na fedha zako zinakwenda wapi?

Huna budi sasa kutunza pesa zako kwa kumbukumbu na kuwa na vitabu muhimu ambavyo vitakusaidia kuweka rekodi na hasa bajeti.

Vitabu muhimu ambavyo unatakiwa kuwa navyo ni:-

(a) Kitabu cha mapato na matumizi

(b) Kitabu cha kuonesha ukwasi

(c) Kitabu cha bajeti

3. Jiwekee vyanzo vingi vya fedha.

Kuwa na vyanzo vingi vya fedha, yaani kuwa na miradi mingi ambayo haikutegemei mpaka uwepo katika utendaji itakusaidia wewe kukupa muda wa kutosha kwa ajili ya kufikiri mipango mipya na udhibiti. Hata pale miradi yako inapokuwa inaenda kombo au vibaya inakuwa ni rahisi sana kutambua.

Vitega uchumi ambavyo utakuwa navyo vitakusaidia sana kuongeza pato lako Na vitakupa pesa kwa ajilii ya matumizi ya leo na maisha yako ya baadae utakapokuwa mtu mzima zaidi.Hii itakusaidia ukiwa uzeeni hutaendelea kufanya kazi bali utaangalia vitega uchumi vyako tu.

4. Tunza mtaji wako.

Utakuwa hufanyi chochote cha maana kama utakuwa unapunguza mtaji wako. Kama umepata hasara katika biashara zako na unaona hasara hiyo inaweza kukata mtaji wako, basi hakikisha unakata gharama zisizo za lazima ili faida ndogo inayopatikana iweze kufidia hasara inayotaka kukata mtaji wako.

Usiwekeze kwa pupa fanya kwanza uchunguzi ukishaona biashara inalipa ndo ufanye au nenda kawaulize wataalam wanaoijua hiyo biashara.

kitabu kava tangazo

5. Uwe makini unapokopesha.

Angalia unapokopesha usikopeshe wasiokopesheka. Kukopesha isiwe fimbo ya kujipigia mwenyewe.Siyo lazima ukopeshe hata kama kuna ahadi na dalili nzuri za kulipwa kwa riba kubwa.

6. Lipa kodi kwa uangalifu sana

Gharama inayosumbua sana ni kodi. Kwa walio wengi kodi inakadiriwa kufika asilimia zaidi ya thelathini ya mapato apatayo mtu. Mfano zipo kodi za aina mbalimbali kama vile kodi ya mapato,kodi ya mauzo,kodi ya mafuta/umeme, kodi ya nyumba na nyinginezo nyingi.Kama utafanikiwa kuokoa kiasi cha asilimia hamsini ya kodi unayolipa sasa kweli utakuwa na fedha nyingi sana ambayo itakusaidia kuwekeza.

Kimahesabu ili tuweze kuwa matajiri tunashauriwa kuwa hatuna budi kulipa kodi ya asilimia kumi ya mapato yetu.

7. Ongeza uwezo wa kuendelea kupata pesa.

Ni watu wachache wanaosoma baada ya kumaliza shule. Kama utaacha kuunoa ubongo wako kabisa lazima ujue utakwama.Lazima kuunoa ubongo wako kila wakati kwa kujisomea,kushiriki kwenye semina, na mambo kama hayo. Usiposoma ubongo wako utaota kutu na kamwe hutasonga mbele kwani itafika wakati utashindwa kukabiliana na changamoto hata ndogo tu.

Uwezo wa kufanikiwa na kufika pale zaidi ya ulipo unao, unaweza ukatumia kanuni hizo kama msingi wa kujijengea namna yakutengeza pesa zaidi binafsi kanuni zingine utaendelea kujifunza hapa hapa katika mtandao huu kwani elimu haina mwisho, nakutakia mafanikio mema.

UNAWEZA KUWASILIANA NA MWANDISHI WA MAKALA HII IMANI NGWANGWALU KWA 0767048035.

KAMA NA WEWE UNA MAKALA NZURI ULIYOANDIKA NA UNAFIKIRI INAWEZA KUWAAMSHA WATANZANIA TAFADHALI NITUMIE KWENYE amakirita@gmail.com

MAKALA ISIWE IMEWEKWA KWENYE BLOG AU CHOMBO KINGINE CHA HABARI, IWE IMETUMIA KISHWAHILI RAHISI NA KINACHOELEWEKA NA IWE NA MANENO KATI YA 500 NA 1000 KARIBU SANA.