Mara nyingi linapokuja suala la kutafuta mafanikio wengi huwa wanalitazama kwa mitazamo tofauti sana. Kuna wanaoamini mafanikio ni kama bahati wakimaanisha kuwa pasipo kuwa na bahati fulani kufanikiwa ni kitu ambacho hakiwezi kutokea kwao. Pia wapo wanaomini na kuhusisha mafanikio ni lazima yatokane na nguvu fulani za ziada. Watu hawa wanaamini sana pasipo kuwa na nguvu hizo mafanikio hayawezekani.
 

Ni kweli inawezekana ukapata mafanikio kupitia nguvu hizo kama unavyojaminisha wewe, lakini kitu cha kujiuliza hapa nguvu hizo unazofikiri zitakupa mafanikio zimekufanikisha kwa kiasi gani ama umekuwa ukipoteza muda kwa kuwa muumini mzuri wa kitu ambacho Hukijui na hakikusaidii? Jaribu kujiuliza tokea umeanza kuamini juu ya bahati, nyota na hata uchawi umeweza kubadilisha maisha yako kwa kiasi gani?
Ni kitu kilichowazi kabisa kuwa watu watu wengi sana ambao ninaweza kusema wameathiriwa kwa sehemu kubwa kwa kuamini kuwa zipo nguvu zilizo nje yao ndizo zinazoweza kuwafanikisha tu na matokeo yake  kushindwa kujiamini wao kama wao. Kati ya nguvu ambayo inaaminiwa na wengi ni nguvu ya uchawi na ambayo ndiyo ningependa tuizungumzie zaidi katika makala hii ya leo.
Tunapozungumzia uchawi ni nguvu pekee ambayo inatumiwa kwa kiasi kikubwa na wengi katika kutafuta mafanikio. Ukiangalia kwa makini katika jamii zetu, utagundua kuwa wafanyabiashara wakubwa, viongozi, wasanii, wanamichezo na wananchi wengi humiminika kwa waganga kutafuta uwezo utakaowapa mafanikio kwenye shughuli zao. Wengine wanaamini bila waganga hao, wao hawana uwezo wa kufanya chochote.
Kwa wengi  kujikuta wanaamini nguvu hizi sana ndivyo wanajikuta kuwa watu wa kupoteza uwezo wao halisi ambao wangeweza kuutumia kutafuta mafanikio na badala yake kukaa tu kusubiri miujiza ambayo huwa mara nyingi haileti manufaa ya muda mrefu, zaidi ya kupoteza muda tu. Kwani kile unachoambiwa ufanye na mganga ndicho hicho hata wewe katika mazingira ya kawaida ukikifanya ni lazima ufanikiwe.
Tuchukulie kwa mfano kwa kuamini nguvu hizi ambazo ziko nje yako ama kwa kuamini uchawi mganga wako amekuambia ili uweze kufanikiwa katika jambo hili ni lazima usile nyama na pia ni muhimu kwako kuamka mapema nyumbani kabla ya mtu yeyote na kuelekea kazini. Nini maana yake? Hicho unachoambiwa ni kitu cha kawaida kabisa ambacho hata wewe ukikifanya uwezo wa kufanikiwa utakuwa nao na ni lazima utafanikiwa. Hapo kilichotumika ni saikolojia ya kawaida kabisa.
Kitu pekee unachotakiwa kufanya ili kuweza kuepukana na imani ambazo sio za lazima kwako, ambazo hata pengine zinaweza zikawa ni mzigo kwako ni kujenga nguvu ya kujiamini ndani mwako. Hii ndio silaha unayotakiwa kuwa nayo ili kufanikiwa kwa chochote kile. Bila kujiamini katika mambo yako huwezi kufanya kitu zaidi utabaki kuwa mnyonge na kuhisi unaonea karibu kwa kila kitu.
Ni muhimu kwako kuweza kubadilisha mwelekeo na kufanya mambo yatakayokupa mafanikio ya kudumu. Utaweza tu kufikia kilele cha mafanikio ukiwa wewe kama wewe, ikiwa utajifunza tabia za watu waliofanikiwa na sifa zao kwa ujumla na sio kung’ang’ana na kitu ambacho hukijui na unalazimishwa ukiamini. Kama utaendelea kuamini juu yanguvu hizi za uchawi kukupa mafanikio  huwezi kufanikiwa.
Unaweza ukajiuliza mmmmh! mbona  kuna watu waliofanikiwa, ni sawa. Lakini mafanikio hayo unayoyaona ni mafanikio ya muda mfupi sana hayafiki popote. Mafanikio halisi ni yale unayoyajenga mwenyewe kwa kuyatengenezea misingi halisi ambayo itakuwezesha kusimama muda wote hata pale mambo yanapoyumba na kwenda vibaya kinyume na matarajio. 
Tunakutakia mafanikio mema, endelea kutembelea AMKA MTANZANIA na KISIMA CHA MAARIFA kujifunza zaidi.
Karibu pia kwenye DIRA YA MAFANIKIO kwa elimu na maarifa bora yatakayoboresha maisha yako.
DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,
IMANI NGWANGWALU,
0713 048035,