Habari za siku rafiki, ni tumaini langu kuwa bado unaendelea kuweka juhudi na maarifa kuhakikisha unafikia malengo ambayo umejiwekea mwaka huu. Hilo ni jambo nzuri na hongera kwa kila hatua ambayo umefanikiwa kuifikia. Karibu tena kwenye Makala hii tuendelee kushauriana mambo mbalimbali yanayohusu maendeleo na uwekezaji wa ardhi na majengo. Katika safari hii wapo baadhi ya marafiki wanapitia changamoto mbalimbali zinazohusiana na uwekezaji huu kutokana na sababu mbalimbali ambazo wengi wao ni kwa sababu ya kukosa maarifa sahihi. Leo nitazungumzia mambo muhimu ya kuzingatia ili kuifanya nyumba yako kuwa bora na salama wakati wote. Hapa nazungumzia uimara wa nyumba kuweza kumudu mazingira kwa muda mrefu pasipo kufanyiwa marekebisho yasiyo na ulazima wowote. Nyumba ni matokeo ya ubunifu na usanifu wa mambo mbalimbali ambayo yanatimiza kiu ya matumizi, ubora na mwonekano uliopo. Ili kuyatimiza haya yafuatayo yanapaswa kuzingatiwa kabla ya ujenzi, wakati wa ujenzi na baada ya ujenzi ili kuifanya nyumba yako kuwa mahali salama na yenye hamasa ya matokeo mazuri ya juhudi zako.


  1. ZINGATIA UBUNIFU NA USANIFU WA NYUMBA

Hii ni hatua muhimu sana kwa yeyote mwenye lengo la kujenga nyumba kwa matumizi yoyote. Hii ni hatua ya lazima kwa wahandisi na wanasayansi wote wa ujenzi ambayo huitumia kuweka lengo na aina zote za mikakati ili kufikia malengo ya ubunifu, usanifu na ujenzi. Hapa unapaswa kuwa na picha halisi ya aina gani ya nyumba unayoitaka, weka sifa na vigezo vyote unavyotaka viwepo katika hali ya mwonekano na matumizi. Ni muhimu sana kuondoa hofu na hali ya ubabaishaji au kutokuwa na hakika kwa kile unachotaka. Hatua hii huongozwa na taarifa zilizo sahihi na zenye uhakika pasipo na shaka ya aina yoyote. Kukosekana kwa usahihi wa taarifa muhimu lazima kutaleta matokeo mabaya wakati na baada ya ujenzi. Mara nyingi nimeona nyumba zikianza kufanyiwa marekebisho muda mfupi sana baada ya kukamilika kwa ujenzi, wanabadilisha kila wanachokiona ni tofauti na matarajio au ushawishi fulani, wanapunguza au kuongeza sehemu ya nyumba ili ikidhi malengo fulani. Mambo haya huleta athari mbaya kwenye ubora wa nyumba. Kitendo hiki ndicho huathiri ubora wa nyumba na kuanza kushindwa kuhimili mazingira. Na sababu kubwa ni kutokuwa na dira ya aina gani ya nyumba unayoitaka, hautaifurahia na kila mahali utaona ni tatizo. Hakikisha unakuwa timamu unapokutana na msanifu majengo na unapata kile ambacho unastahili, usimuache msanifu majengo akutengenezee ramani ya mtazamo wake peke yake, atakupa ramani ya nyumba ya ndoto yake na siyo yako, utaikinai baada ya muda mfupi sana kwa kuwa haitakuwa na baadhi ya wasifu unaoupenda.

  1. ZINGATIA UBORA WAKATI WA UJENZI

Hapa nazungumzia ubora wa malighafi utakazotumia, ubora wa mafundi na wasimamizi, ubora wa mbinu zitakazotumika wakati wa ujenzi na ubora wa vifaa au vitendea kazi. 

Umakini wa viwango vya juu sana unahitajika katika kufanikisha ubora wa nyumba unafikia viwango vya kitaalamu. Uhakiki wa rasilimali zote zinazotumika wakati wa ujenzi lazima uzingatiwe, kuhakikisha usanifu wa kitaalamu unazingatiwa na muhimu zaidi ni kufanya upembuzi yakinifu kwa kila hatua ya ujenzi ili kuepuka upotevu wa rasilimali za ujenzi na muda. Ushirikiano na mawasiliano mazuri kati yako na wataalamu wa ujenzi ndio nguzo pekee itakayoleta matokeo mazuri na yenye ubora kwenye nyumba yako. Kwenye hatua hii utaepukana na nyufa, fangasi, mchwa na matatizo yote yenye athari kwenye majengo. Maamuzi na ushauri wowote utakao tekelezwa kwenye hatua hii ndio utakao amua ubora wa nyumba ya ndoto yako. Tafakari, Utimamu wako ndio ubora wa nyumba yako.

  1. EPUKA MATUMIZI MABAYA YA NYUMBA

Ubunifu na usanifu wa nyumba huzingatia sana matumizi husika ya aina ya nyumba unayoitaka kuijenga. Matumizi husika ya nyumba huwa ni sehemu ya dira kwa wataalamu wote wa ujenzi katika ubunifu, usanifu na mpangilio wa malighafi wakati wa ujenzi. 

Usifanye matumizi ya jikoni tofauti na jikoni, usigeuze chumba cha kulala kuwa sehemu ya kufulia, usigeuze nyumba ya kuishi kuwa karakana na mengine mengi yanayofanana na haya. Usibadili matumizi pasipo kupata ushauri wa wataalamu wa ujenzi na wa fani husika kwa matumizi unayotarajia kutumia. Mfano unataka kubadili nyumba ya kuishi kuwa nyumba ya biashara, zahanati au shule, unapaswa kuzingatia kama hiyo nyumba inaweza kumudu hayo mabadiliko pasipo kuathiri ubora. Fikiria kuhusu matumizi na zingatia aina ya malighafi zilizotumika kama zina uwezo wa kuhimili matumizi mapya pasipo athari yoyote kwenye ubora na muundo. Kuna baadhi ya marafiki hata kuweka vilainishi kwenye bawaba za milango huwa ni tatizo sugu, hata swichi za umeme zina zaidi ya miaka iliyoamriwa kutumika lakini hawataki kubadilisha hadi zilete majanga. 

Nyumba inapaswa kutunzwa ili iendelee kukutunza na kupunguza gharama za matengenezo yasiyo na ulazima wowote.

  1. IKINGE NYUMBA YAKO DHIDI YA MAJANGA

Nyumba ni kama kiumbe chochote ambacho ni sehemu ya mazingira, ili nyumba iendelee kuwa bora na salama ni lazima iwe na uwezo wa kupambana na hatari zote za kimazingira ziwe za asili au zinazotokana na matumizi ya kibinadamu. Majanga kama ya moto, mafuriko, matetemeko ya ardhi, kimbunga, milipuko, mizizi ya miti na chemikali au matendo mbalimbali ya kibinadamu. Ni muhimu sana kufanya upembuzi yakinifu kuhusu hatua mbalimbali za kukabiliana na hatari hizo ili uweze kuchukua hatua za haraka kadri unavyoweza. Wahandisi na wanasayansi wa ujenzi huzingatia sana ubora wa malighafi zenye uwezo wa kuhimili majanga na kuweka miundombinu rafiki ya kuweza kupambana na majanga hayo. Hivyo na wewe rafiki unapaswa ujiulize, endapo utakabiliwa na aina yoyote miongoni mwa janga, je upo uwezekano wa wewe kuepuka au nyumba yako kushindwa kabisa kuhimili au kutopata athari zilizopitiliza. Tafakari sana, fahari ya nyumba ni ubora na maisha yana thamani sana unapokuwa upo salama.

Tafakari yako kuhusu Makala hizi ni muhimu sana…..!!!! maoni na maswali yako ni mambo ambayo nayazingatia sana. Usisite kuwasiliana nami endapo dhamira yako itakusukuma kufanya hivyo. Karibu sana.

Tuendelee kuwa pamoja kupitia AMKA MTANZANIA tufike kwenye kilele cha mafanikio, pia endelea kufuatilia makala zijazo ili ujifunze zaidi.

Mwandishi wa makala hii ni mwanataaluma wa ujenzi.

Anapatikana kwa: Simu: +255 685 729 888


Baruapepe: kimbenickas@yahoo.com