Rafiki yangu mpendwa,
Unapomuona mtu ambaye ana utajiri na mafanikio makubwa, ni rahisi sana kujipa sababu mbalimbali zilizomfikisha hapo.
Unaweza kusema ametokea kwenye familia yenye uwezo mkubwa, au ana akili sana au mazingira yake yamembeba.
Lakini unawezaje kuelezea haya?
Kwenye familia moja, bado kuna watu wanakuwa matajiri na wengine kuwa masikini. Kama hali ya familia ingekuwa sababu, si wote wangekuwa sawa?
Kwenye kila aina ya kazi na biashara, kuna watu wanakuwa matajiri na wengine wanakuwa masikini. Kama kazi au biashara ingekua sababu si wote wangepaswa kuwa sawa?
Vipi wale wanaoshinda bahati nasibu na kupata fedha nyingi kwa wakati mmoja, lakini baada ya muda mfupi wanakuwa wamepoteza fedha zote na kurudi walipokuwa kifedha? Kama tofauti ya matajiri na masikini ingekuwa fedha, wanaozipata kwa wingi wangekuwa wamejikomboa kabisa.
Unawajua wengi ambao walipata mafao au uridhi wa mali lakini baada ya muda mfupi wakawa wamepoteza kila kitu na kurudi pale walipokuwa kifedha.
Rafiki, kwa mifano hiyo iliyo wazi kabisa kwenye jamii zetu, ni dhahiri kwamba tofauti ya matajiri na masikini siyo kile tunachoona kwa nje.
Siyo familia, mazingira, kazi, biashara au fedha.
Chochote kinachoonekana kwa nje, siyo kinachowatofautisha matajiri na masikini.
Bali kuna kitu kisichoonekana ambacho ndiyo kinazalisha tofauti hiyo kubwa.
Rafiki, tofauti ya matajiri na masikini inaanzia kwenye akili.
Hicho ndiyo mwandishi T. Harv Eker anatufundisha kwa kina kwenye kitabu chake kinachoitwa SECRETS OF MILLIONAIRE MIND.

Kwenye kitabu hicho, Eker ameshirikisha kanuni ya uumbaji ambayo iko ndani yetu na ndiyo inayozalisha kila matokeo tunayopata.
Kanuni hiyo ni; M –> F –> H –> T –> K
M ni mtazamo ambao mtu anakuwa nao, huu unajengwa kwa imani ambazo mtu anakuwa amejijengea yangu utoto wake.
F ni fikra ambazo zinatokana na mtazamo mtu alionao.
H ni hisia ambazo zinachochewa na fikra anazokuwa nazo mtu.
T ni hatua ambazo mtu anachukua kutokana na hisia anazokuwa nazo.
K ni matokeo ambayo mtu anayapata.
Watu wengi wamekuwa wanakazana kubadili matokeo ya mwisho bila kubadili vitu hivyo vingine na kinachotokea ni wanashindwa kubadilika.
Eker anatuambia kama tunataka mabadiliko ya kweli, lazima tuanze kwa kubadili mtazamo na imani tulizonazo.
Na inapokuja kwenye swala la fedha, kuna imani 17 potofu ambazo zimekuwa ndiyo kikwazo kikubwa kwa wengi kupata utajiri.
Imani hizo 17 ndiyo zinazowatofautisha matajiri na masikini.
Kwa kuzijua na kuzivunja imani hizo 17, huwezi kubaki hapo ulipo sasa.
Je upo tayari kwenda viwango vya juu zaidi ya hapo ulipo sasa?
Kama jibu ni ndiyo basi nakukaribisha kwenye mjadala wa moja kwa moja wa kitabu hiki cha SECRETS OF MILLIONAIRE MIND.
Mjadala huo utafanyika leo jumamosi tarehe 14/08/2021 kuanzia saa mbili kamili usiku saa za Afrika Mashariki.
Unaweza kushiriki mjadala huu ukiwa popote duniani, kushiriku fungua kiungo hiki; https://t.me/somavitabutanzania?voicechat
Rafiki yangu mpendwa, usikubali kuendelea kubaki kwenye umasikini wa kujitakia.
Njoo kwenye mjadala leo uweze kufungua mtazamo wako na kubadili fikra zako kitu kitakachobadili sana matokeo unayoyapata.
Ukiendelea kufanya unachofanya sasa, utaendelea kupata matokeo ambayo umekuwa unapata.
Ukitaka kupata matokeo ya tofauti, lazima ufikiri na kufanya vitu vya tofuati.
Karibu kwenye mjadala wa leo ili uweze kuwa tofauti na uzalishe matokeo ya tofauti.
Rafiki yako anayekupenda sana,
Muuza Matumaini Kocha Dr Makirita Amani
http://www.somavitabu.co.tz