3079; Hapana sahihi kwako.

Rafiki yangu mpendwa,
Kama ambavyo tunajua, tupo kwenye msimu wa kusema HAPANA.
Ni msimu wa kupeleka umakini na juhudi zote kwenye vitu vichache na kuachana na vingine vyote.

Watu hudhani kusema hapana ni rahisi sana, kwa sababu vitu unavyokataa ni ambavyo huvitaki.
Lakini hilo siyo sahihi.
Hapana sahihi kwako ni ile inayokuuma kusema.

Hapana unayofurahia kuisema ni ile ambayo inahusisha kitu ambacho hukuwa unakihitaji kabisa.
Na hivyo ni kitu ambacho hakikuwa na madhara kabisa.

Hapana inayoumiza kuisema ni ile ambayo inahusisha kitu ambacho unakipenda na kukikubali sana na pia upo vizuri kwenye kukifanya.
Ni kitu kinachokuuma kuacha kufanya kwa sababu kina fursa ya kufanya makubwa zaidi.

Hapana sahihi kusema, ambayo pia inaumiza kusema ni ile unayosema kwa vitu ambavyo umeshapata mafanikio fulani.
Yaani ni sawa na kuwaua baadhi ya watoto wako ili ubaki na wachache ambao watafany vizuri zaidi.

Hiki ni kitu ambacho wakulima wanakielewa kwa asili.
Wakati wa kutunza mazao yao, huwa wanalazimika kupunguza baadhi ya matawi au matunda yaliyoanza kutokeza ili kubaki na machache yatakayokuwa bora zaidi.

Kwa mtu mgeni kwenye kilimo, akiona matawi mengi yenye maua anaona atapata mazao mengi. Anayatunza yote asipoteze hata moja.
Matokeo yake anapata mazao mengi lakini yaliyo hafifu, yanakuwa madogo na yasiyo na ubora.

Kwa mkulima mzoefu anajua kadiri mche mmoja unavyokuwa na maua mengi, ndivyo mazao yanayozalishwa yanavyokuwa hafifu.
Hivyo hupunguza matawi hayo haraka sana ili kubakiza machache ambayo yatazalisha mazao bora sana.

Tukifananisha na masomo, ni sawa na mwanafunzi anayechukua masomo matano na kupata wastani wa B kwenye masomo yote, huo ni ufaulu mzuri.
Lakini ukilinganisha na mwanafunzi mwingine anayechukua masomo mawili na kupata wastani wa A kwenye masomo yote, huo ni ufaulu bora zaidi.

Mambo yote yanayokuwa rahisi kufanya ni ambayo hayana mchango kwenye mafanikio yako makubwa.
Na mambo yote yanayokuwa magumu kufanya ndiyo yenye fursa ya kukupa mafanikio makubwa.

Ili upate mafanikio makubwa, lazima uwe tayari kutoa kafara vitu ambavyo umekuwa unavifanya vizuri na hata kuvipenda, ili kukusanya nguvu zako kwa vitu vilivyo bora zaidi.

Ni bora kuchimba kisima kimoja kwa urefu mkubwa zaidi kuliko kuchimba visima vingi kwa urefu mdogo.
Nguvu zile zile unazotawanya kwenye mashimo mengi, ndizo ambazo ukizikusanya kwenye shimo moja litakuwa refu sana na hivyo kukupa matokeo makubwa.

Kitu kinavyokuwa kigumu kwako usikikimbie, kina ugumu kwa sababu ndani yake kina fursa kubwa.
Kutokana na ugumu wake, kila mtu anakimbia kukifanya.
Hivyo basi, ukikifanya wewe, unakuwa mbele zaidi ya wengine na hivyo kupata manufaa makubwa.

Kagua vitu vyote unavyovifanya kwa muda wako na ona ni wapi unapotawanya nguvu ambazo ungezikusanya zingezalisha matokeo makubwa na bora zaidi.
Hili ni zoezi la kufanya mara kwa mara kwa sababu huwa ni rahisi sana kujisahau na kutoka kwenye mchakato mkuu unaokuwa nao.

Moja ya kazi kubwa kwenye safari yako ya mafanikio ni kujirudisha kwenye njia kuu. Kabla hujaongeza kasi kwenye yale unayofanya, ni muhimu sana kuhakikisha ni sahihi kuyafanya.

Sema HAPANA kwenye mambo mazuri kwako kufanya ili uweze kusema NDIYO kwenye mambo ambayo ni bora zaidi kwako kuyafanya.
Na kama HAPANA zako hazikuumi wewe binafsi, jua hizo siyo hapana sahihi kwako.

#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji
#BilioneaMafunzoni
#NajengaBiashara
#HakunaKingineMuhimu
#LazimaNitoboe
#NawekaKaziNifanikiwe