3169; Msukumo wa kufanya maamuzi.

Rafiki yangu mpendwa,
Kama kuna kitu ambacho watu huwa wanakikwepa sana ni kufanya maamuzi.
Kama kuna nafasi ya watu kusubiri kufanya maanuzi, wataitumia kusubiri.

Unaweza kuona ni jambo la kistaarabu kuwaacha watu mpaka wawe tayari kufanya maamuzi wao wenyewe.
Lakini inapokuja kwenye mambo muhimu, hupaswi kuwa hivyo.

Kwa mfano kwenye mauzo, unaweza kumweleza mteja kuhusu kile unachouza, akaelewa vizuri. Lakini akakuambia nitakutafuta nikiwa tayari.
Ukisikiliza kauli hiyo unaweza kujipa matumaini kwamba mteja atakutafuta.
Lakini unajua kwa uzoefu, wateja wakikuambia watakutafuta, huwa ni nadra sana kufanya hivyo.

Kwenye mauzo ni wajibu wako muuzaji kuwasaidia wateja kufanya maamuzi ya kununua.
Hiyo ni kwa sababu maamuzi ya kununua ni maamuzi makubwa sana.
Ni maamuzi yanayowatenganisha watu na fedha zao, kitu ambacho wengi huwa hawapendi kukiendea kwa haraka.

Lakini pia wakati unawasubiria wateja wawe tayari kufanya maamuzi, wakikutana na muuzaji mwingine ambaye amejipanga vizuri kwenye eneo la mauzo, huwa wanaishia kununua.
Wanakuacha wewe na ahadi nzuri waliyokupa.

Ili uwasaidie watu kufanya maamuzi, ni lazima uwawekee msukumo kwenye kufanya hivyo.
Na kwenye mauzo, kuna vitu vinne unavyopaswa kufanya kuwasukuma wateja kufanya maamuzi.

Kitu cha kwanza ni UHABA.
Uhaba ni pale ambapo vitu vinapatikana kwa uchache wakati uhitaji ni mkubwa.
Watu wanapoona kuna uhaba wa kitu, huwa wanasukumwa kuchukua hatua mara moja ili wasikose.
Kwa chochote unachouza, waonyeshe watu uhaba uliopo, ambao ni wa kweli na hilo litakuwa msukumo mkubwa kwao kuamua badala ya kuendelea kusubiri.

Kitu cha pili ni UKOMO.
Ukomo ni pale ambapo muda wa kufanya maamuzi unapokuwa mdogo.
Kwenye ukomo kunakuwa na muda ambao watu wanaweza kuchukua hatua. Baada ya muda huo kupita wanakuwa hawawezi tena kufanya maamuzi hayo.
Kadiri muda wa kufanya maamuzi unavyokuwa mdogo, au muda unavyokaribia mwisho, ndivyo watu wanapata msukumo mkubwa wa kufanya maamuzi.

Kitu cha tatu ni NYONGEZA.
Nyongeza ni pale unapompa mtu vitu vya ziada ili aweze kufanya maamuzi mara moja. Kwa kuongeza vitu, watu wanaona thamani ni kubwa kuliko bei na hilo linawasukuma wafanye maamuzi mara moja badala ya kuendelea kusubiri.
Watu wengi wamekuwa wanasubiri kwa sababu wanaona thamani wanayopata ni ndogo kuliko bei wanayopaswa kulipia.
Hata pale watu wanapokutaka upunguze bei, ukiwaongezea thamani zaidi wataikubali bei.

Kitu cha nne ni UHAKIKA.
Uhakika ni pale unapompa mtu imani kwamba akifanya maamuzi hawezi kupoteza. Kitu kinachowafanya wengi wasubiri kwenye ufanyaji wa maamuzi ni kukosa uhakika. Watu wanapoona kuna hatari ya kupoteza huwa wanasubiri kufanya maamuzi na kuchukua hatua.
Unapowapa uhakika kwamba kwa maamuzi watakayofanya hawawezi kupoteza, wanasukumwa kufanya maanuzi.
Wape watu uhakika wa kupata bidhaa/huduma nyingine au kurejeshewa fedha pale kile wanachokuwa wamenunua hakijawafaa kama walivyotaka.

Rafiki, mambo hayo manne yanagusa hisia kuu mbili zinazowasukuma watu kuchukua hatua.
Moja ni hofu ya kupoteza, ambapo uhaba na ukomo ndivyo vinagusa hisia hiyo. Vinawafanya watu waone watapoteza kama hawatafanya maamuzi na hapo wanasukumwa kuamua mara moja.
Mbili ni tamaa ya kupata, ambapo ziada na uhakika vinawafanya watu waone wanapata manufaa kitu kinachowasukuma kuamua mara moja.

Kwenye hisia za kufanya maamuzi, hofu ina nguvu kubwa kuliko tamaa.
Hivyo uhaba na ukomo huwa vina nguvu kubwa zaidi pale vinapotumiwa vizuri.

Lakini pia, pale hofu na tamaa vinapotumika kwa pamoja, nguvu yake huwa inakuwa kubwa zaidi.
Hivyo kama unaweza kutumia vitu vyote vinne kwa mteja mmoja, na ikawa kweli kabisa, hakuna namna mteja ataacha kuchukua hatua mara moja kama kweli ana uhitaji na anaweza kumudu kulipia.

Mfano, kwa kumwonyesha mteja bidhaa zimebaki chache (uhaba), kuna ofa umempa (ziada) ambayo itaisha ndani ya siku moja (ukomo) na kama bidhaa hazitafanya kazi ataweza kurudisha (uhakika) mtu lazima atafanya maanuzi.

Kwenye mauzo, ustaarabu siyo kuwasubiri wateja mpaka wawe tayari kufanya maamuzi wao wenyewe.
Bali kwenye mauzo ustaarabu pekee ni kukamilisha mauzo mapema.
Na utaweza kufanikisha hilo kwa kuwasukuma wateja kufanya maamuzi mara moja badala ya kusubiri kwa muda mrefu.

Na kwa kuwa kile unachouza unajua kabisa kina manufaa kwa wateja unaowashawishi, wanakihitaji na wanaweza kukimudu, usihofie kuwasukuma kufanya maamuzi.
Kwani watakushukuru sana baadaye kwa manufaa makubwa wanayokwenda kuyapata.

#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji
#BilioneaMafunzoni
#NajengaBiashara
#HakunaKingineMuhimu
#LazimaNitoboe
#NawekaKaziNifanikiwe