3188; Ni milioni tu.

Rafiki yangu mpendwa,
Mwenzetu hapa, Martin Tindwa, anaandika kitabu ambacho anakiita Jilipe Wewe Mwenyewe.
Ni kitabu kuhusu mpango binafsi wa kifedha wa kujilipa wewe mwenyewe kwanza kwenye kila kipato ambacho mtu unaingiza.

Kwenye kitabu hicho, Martin kuna dhana moja muhimu sana ambayo ameizungumzia na ina uzito mkubwa sana inapokuja kwenye kujilipa mwenyewe na kuwa na akiba ya dharura.
Dhana hiyo ni kwamba matatizo mengi ya kifedha ambayo yanawasukuma watu kwenda kukopa fedha yako chini ya shilingi milioni moja.

“Matatizo mengi madogo madogo kwenye maisha ambayo yanatusumbua sana yapo chini ya shilingi milioni moja. Ndiyo maana mara nyingi watu wamekua wakikopa pesa ndogo chini ya milioni moja ili kukabiliana na changamoto za dharura ambazo zimekuwa zikijitokeza mara kwa mara na hivyo kupelekea changamoto madeni kuzidi kujitokeza kwenye maisha yao.” – Martin Tindwa

Dhana hii ambayo ni ya kweli kabisa inaonyesha jinsi ambavyo watu wengi wenye matatizo ya kifedha wanakuwa wamejitakia wao wenyewe kwa kukosa akiba kidogo tu za dharura ambazo hazizidi milioni moja.

Yaani kama watu wengi wangeweza kuwa na kiasi cha fedha kisichopungua milioni moja kwa ajili ya dharura ndogo ndogo zinazoweza kujitokeza kwenye maisha yao, wasingejikuta kwenye mikopo ambayo inawasumbua sana.

Hizo kelele tunazosikia za wakopeshaji wasio rasmi wanaowaumiza watu kwa riba kubwa na vikundi vya kukopeshana fedha kwa masharti makali maarufu kama ‘kausha damu’ ni kwa sababu tu watu wameshindwa kujijengea nidhamu ya kujilipa wao wenyewe kwenye kila kipato wanachoingiza.

Tatizo la umasikini huwa ni la kiakili zaidi kuliko kifedha, ndiyo maana ukitaka uchukiwe na masikini, waambie ukweli ambao unawaumiza.
Kwa mfano ukisema mtu yeyote ambaye anafanya shughuli yoyote ya kumwingizia kipato ila hana akiba ya dharura ya shilingi milioni moja hayupo makini na maisha yake, walio kwenye hali hiyo watachukizwa sana na hilo.

Watakulalamikia jinsi ambavyo kipato wanachoingiza ni kidogo na hakitoshelezi.
Watakuambia jinsi ambavyo kila wakijaribu kuweka akiba mambo yanaingilia na kujikuta wametumia.
Watakuambia mengi sana, ambayo kama utawasikiliza, unaweza kuwaonea huruma na kudhani kweli kwamba mambo ni magumu sana kwao.

Lakini kama utataka kujisumbua na kupitia matumizi yote ya mtu ndani ya miezi 12 iliyopita, yote kabisa bila kuacha hata moja, utapata matumizi yasiyo ya msingi kabisa ya zaidi ya shilingi milioni moja kwa mwaka.
Unajua watu wanapenda fedha, ila hawapendi hesabu.
Ukigawa shilingi milioni moja kwa siku za mwaka unapata wastani wa kama elfu 3 hivi kwa siku.

Ukiyamulika maisha ya wengi ambao wanakosa milioni moja kama akiba ya dharura, kuna elfu 3 nyingi wanazopoteza kila siku kwa matumizi yasiyo ya msingi kabisa.
Labda ni kula milo mitatu ya siku ambayo haina umuhimu wowote.
Au kulipia usafiri wa haraka kama wa pikipiki ambao haukuwa na ulazima.
Au kununua vocha kwa ajili ya kuingia mitandaoni na hakuna fedha ambayo mtu anaingiza kupitia mitandao hiyo.
Au kununua nguo wakati mtu hatembei uchi.
Au kujiburudisha kwa vinywaji kama soda au pombe wakati maji yangetosha.
Au kununua maji wakati ya bure ya kuchemsha yangewafaa.

Sina shaka kabisa kwamba mtu yeyote mzima anayekosa akiba ya dharura ya shilingi milioni moja ni mzembe.
Hama tatizo sana la fedha, bali ana tatizo la kukosa umakini zaidi.

Wakati nafikiria kushirikisha dhana hii kwenye hizi kurasa zetu za kila siku, nilijiambia hii ni ya chini kwa watu tuliopo hapa, yaani watu tunaozungumzia ubilionea awepo ambaye akiba ya dharura ya milioni imshinde?
Niliamini hilo haliwezekani, hasa kwa vile ambavyo wengi wamekuwa kwenye hii huduma kwa muda mrefu.
Na pia kwa sababu kitabu kikuu cha fedha ambacho kila mtu hapa amekisoma, kilitoka zaidi ya miaka mitano iliyopita na kitabu hicho kimeeleza kwa kina dhana ya kujilipa mwenyewe na jinsi ya kufanya hivyo.

Lakini baada ya kupitia taarifa za uwekezaji wa UTT za watu karibia wote walio kwenye hii programu, nimeshtushwa sana na idadi kubwa ya watu ambao jumla ya uwekezaji wao wa UTT ni chini ya milioni moja.
Hawa ni watu ambao kwa uhakika hawana akiba ya dharura ya shilingi milioni moja.
Kwa kifupi tunaweza kusema watu hawa wapo kwenye shimo refu sana la kifedha ambalo hawakupaswa kuwepo kabisa.

Hivyo tutakapoanza kuwapunguza watu kwenye programu hii, tutaanza na wale ambao hawana uwekezaji kabisa wa UTT au uwekezaji wao mpaka kufikia mwezi Agosti 2023 ulikuwa chini ya shilingi milioni moja.

Sawa, hiyo imekuja kwa ziada tu.
Kwenye ukurasa huu wa leo masomo makuu yalikuwa mawili;
Moja ni matatizo mengi ya kifedha ambayo watu wanasumbuka nayo ni ya fedha ndogo ndogo.
Na mbili, wengi wanaosumbuliwa na matatizo ya fedha ndogo ndogo siyo kwa sababu wanazikosa, ila kwa sababu wanakosa umakini.

Kwa nyongeza tu, kama utaikosa programu kwa sababu ya kukosa vigezo mbalimbali ambavyo vitaelezwa ondoka na hasira ya kwenda kufanyia kazi mpango wa LAKIONEA ambao tumewahi kushirikishana hapa (https://www.kisimachamaarifa.co.tz/2023/08/05/3139-dola/).
Kapambane huko uwezavyo mpaka ufikie ngazi hiyo ya LAKIONEA na ukija tena nitakupokea kwa mikono miwili kwenye programu ya Bilionea Mafunzoni.
Lakini chini ha hapo, pambana na programu nyingine ambazo nitakupa nafasi, kama programu ya CHUO CHA MAUZO.

Kwa mfano ukiamua tu kukomaa na mauzo kwa kiwango cha juu kabisa, ukajipa miaka mitatu ya kupambana usiku na mchana na kufuata mkakati wa LAKIONEA, utaweza kulifikia hilo lengo na kurudi tena kwenye kundi.
Lakini tofauti na hapo, hatutaweza tena kuongea lugha moja.

Kwa kumalizia, kuwa na jumla ya uwekezaji UTT zaidi ya milioni moja siyo kigezo pekee, hicho ni kimoja tu na cha chini kabisa.
Kuna vigezo vingine viwili vya milioni moja na vingine vya kimchakato.
Tutaendelea kushirikishana kadiri muda unavyokwenda.

#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji
#BilioneaMafunzoni
#NajengaBiashara
#HakunaKingineMuhimu
#LazimaNitoboe
#NawekaKaziNifanikiwe