Sikiliza hapa;
Rafiki yangu Mpendwa,
Wakati mwingine sisi binadamu ni viumbe ambao tunachekesha sana. Tunajua kabisa ni nini ambacho tunataka. Tunajua nini tunapaswa kufanya ili tupate tunachotaka. Tunaweka mipango ya kufanya ili tupate tunachotaka. Hayo yote yanakwenda vizuri kabisa na tunakuwa na matumaini makubwa kwamba tunaenda kubadili maisha yetu.
Ni mpaka wakati wa kufanya unapofika ndiyo tunaanza vituko. Mara nyingi tunashindwa kabisa kuanza, hivyo tunaishia kuahirisha na kujiambia tutafanya wakati mwingine. Tukijilazimisha na kuanza kufanya, hatuendi mbali, usumbufu unajitokeza na tunaishia njiani.
Hii inachekesha kama umeshajenga mafanikio makubwa unayoyataka. Lakini kama bado hujayapata mafanikio hayo makubwa, inaumiza. Kwa sababu ndiyo uhalisia ambao tunapambana nao kila siku.
Unaweza mpaka kujishangaa, na kuona labda kuna kitu hakipo sawa kwako. Iweje uweke mipango wewe mwenyewe, lakini ushindwe kuitekeleza? Kwa sababu unajua kabisa kwamba kama ungetekeleza yote uliyowahi kupanga huko nyuma, usingekuwa hapo ulipo sasa. Hata ungetekeleza nusu tu, ungekuwa mbali zaidi ya hapo ulipo.
Kwa wanaoshindwa, wamekubaliana na hali hiyo na kuona hawana cha kufanya. Kwa wanaofanikiwa wanajua kipo cha kufanya, wanakitafuta na kukifanya, kitu kinachowawezesha kupata mafanikio makubwa.
Kwenye barua hii tunakwenda kujifunza njia ya uhakika ambayo itaondolea usumbufu ambao umekuwa unakukwamisha kufanya makubwa kadiri unavyotaka.

1. Andika Maamuzi Yako Kabla Ya Kuchukua Hatua.
Njia itakayokusaidia kuepuka usumbufu na kutekeleza yale uliyopanga ni kuwa na utaratibu wa kuandika kila maamuzi kabla ya kuchukua hatua. Na unayaandika kwa kalamu na karatasi na siyo kwenye simu au kifaa kingine chochote.
Unaweza kujiuliza si ndivyo unavyofanya maamuzi yako, kwa kuandika? Hapana, hii ni tofauti. Ndiyo, unafanya maamuzi kwa kuweka malengo na mipango na kuandika.
Halafu inakuja wakati wa kutekeleza, ambapo unashindwa kabisa kuanza au unaanza lakini unahama na kwenda kwenye jambo jingine. Hapo sasa ndipo unapohitaji kuandika hayo maamuzi kabla ya kuyafanya.
Kwa mfano, kama nimepanga saa tatu mpaka saa sita mchana nitaandika, inapofika hiyo saa tatu naandika kwenye kijitabu changu; ‘kuanzia saa tatu mpaka saa sita naandika, sitafanya kitu kingine.’ Baada ya kuandika naanza kutekeleza.
Kama dakika 10 baadaye nitajiambia inabidi niangalie simu kama kuna mtu ananitafuta au niingie mtandaoni kutafuta kitu fulani, napaswa kuandika kwanza. Hivyo nachukua tena kijitabu changu na kuandika; ‘saa tatu na dakika 10, naingia mtandaoni kuangalia hiki kitu.’ Ni baada ya kuandika ndiyo naweza kuacha nilichokuwa nafanya ndiyo nifanye kingine.
Sasa hapo kuna mambo yatajitokeza, ambayo ndiyo sababu za njia hiyo kufanya kazi vizuri sana;
Moja ni kitendo cha kulazimika kuandika, inafanya kile kinachotutoa kwenye tunachofanya kiwe muhimu sana. Kama siyo kitu muhimu, hilo zoezi la kuandika tu lenyewe linatuonyesha kabisa kwamba tunajipa usumbufu.
Mbili ni kuondoa mihemko ya kufanya vitu vinavyotujia, wakati ambapo tuna kilicho muhimu zaidi mbele yetu. Mara nyingi huwa tunapata mawazo ambayo tunaona ni mazuri sana, lakini yanakuwa usumbufu wa kututoa kwenye kilicho muhimu.
Tatu ni kuweka ukomo kwenye usumbufu, kama kinachotutoa kwenye tunachofanya ni muhimu, hatutajisahau, tutakifanya na kurudi kwenye jukumu kuu. Kwa hali ya kawaida, saa tatu na dakika 10 unajiambia unaingia mtandaoni kutafuta kitu fulani, lakini unakuja kujikuta umetumia zaidi ya saa nzima ukihangaika na vitu vingine. Sasa kwa sababu umeandika unaingia mtandaoni kuangalia kitu kimoja tu, ukishawishika kuangalia kitu kingine ni lazima uandike kwanza. Kwa ulazima wa kuandika, utaona kabisa jinsi unavyopoteza muda na kuzuia hilo lisiendelee kukukwamisha.
2. Kuwa Na Ratiba Ya Siku Nzima, Na Nyakati Zilizo Muhimu Zaidi.
Huenda unajiambia hilo zoezi ni gumu sana. Ina maana hata kama unataka kwenda chooni uandike? Hata kupiga mswaki nako uandike? Ukianza kufikiria hivyo, unajipa sababu ya kushindwa kabla hata hujaanza.
Hili zoezi unapaswa kulifanya kwenye nyakati ambazo umepanga kufanya majukumu muhimu kwa ajili ya mafanikio unayotaka. Siyo zoezi la kufanya kwa masaa yote 24 ya siku, japo ukipenda unaweza kufanya.
Ili uweze kufanya zoezi hili, kwanza unatakiwa kuwa na ratiba ya siku yako nzima, ratiba ambayo unakuwa unairudia kila siku (daily routine). Kwenye ratiba hiyo, unatenga muda ambao ndiyo wa wewe kufanyia kazi mambo yako ya mafanikio.
Kwenye huo muda uliotenga ndiyo utaandika kila unachotaka kufanya, hata kama ni kwenda chooni. Nje ya muda huo, huna ulazima wa kuandika, lakini ukitaka pia siyo mbaya.
Kwa mfano, kwenye siku yangu nina nyakati tatu za kufanya kazi kwa kina, alfajiri (saa tisa mpaka kumi na mbili), asubuhi (saa mbili mpaka saa saba) na mchana (saa nane mpaka kumi na mbili). Kwenye hizi nyakati, ni lazima niandike kila ninachofanya. Muda mwingine nje ya hapo naweza kufanya chochote bila kulazimika kuandika kwanza.
Tengeneza ratiba yako ya kila siku, ambayo utaifuata bila kuivunja na ndani yake ainisha nyakati ambazo ni za kufanyia kazi mipango yako ya mafanikio. Kwenye hizo nyakati, tekeleza yale uliyopanga na andika kila unachofanya kabla ya kukifanya.
Mara zote huwa nakuwa na ratiba ya siku na nimekuwa na orodha ya mambo ninayofanya kwenye siku. Lakini njia hii ya kuandika kwanza kila kitu kabla ya kufanya, nimejifunza na kuanza kuifanyia kazi siku za karibuni. Matokeo yake yamekuwa ni mazuri sana, imenisaidia sana kuondokana na usumbufu ambao huwa unaninyemelea, hasa ninapokuwa nimeanza kuchoka.
Endelea kusoma #BaruaYaKocha kupata njia nyingine tatu za kuhakikisha usumbufu haukukwamishi kufanikiwa.
Soma hapa; #078; Hii Ndiyo Njia Ya Uhakika Ya Kuondoa Usumbufu Unaokukwamisha Kufanya Makubwa