Katika ujasiriamali na biashara kila mfanya biashara anajua kwamba fedha ndio damu ya biashara. Kama hakutakuwa na mzunguko wa fedha wa kutosha kwenye biashara ni sawa na mtu ambaye hana damu ya kutosha na hivyo itapelekea kufa kwa biashara. Na njia kubwa ya kuongeza mzunguko wa fedha kwenye biashara yoyote ni kuongeza mauzo. Hii ina maana kwamba tayari unayo huduma au biadhaa inayohitajika na kwa bei unayouzia unapata faida, hivyo basi utakapouza mara nyingi zaidi utapata faida kubwa zaidi.
Leo tutajadili njia tano unazoweza kutumia kuongeza mauzo kwenye biashara yako. Kupitia njia hizi utaweza kuuza zaidi kwa wateja ulioko nao sasa, kuuza kwa wateja wapya na hata kuwafanya wateja wako waendelee kuwa na wewe.
1. Jenga uhusiano mzuri na wateja wako.
Njia ya kwanza ni kujenga uhusiano mzuri na wateja wako. Biashara za zama hizi zinajengwa kwa uhusiano. Mteja atakuwa tayari kununua bidhaa au huduma kwa mtu ambaye anaona anamjali na anajali mahitaji yake. Kwa mfano kama wewe ungekuwa unataka kununua kitu na kuna wauzaji wawili, mmoja ni rafiki yako na mwingine ni mtu ambaye humjui kabisa, utanunua wapi? Moja kwa moja utanunua kwa rafiki yako kwa sababu unajua hawezi kukuuzia kitu kibaya au kukulaghai. Hivyo basi jenga mahusiano mazuri na wateja wako na wajisikie kwamba wanafanya biashara na mtu ambaye ni rafiki yao. Omba namba zao za simu na mara kwa mara wasiliana nao kuwajulia hali na kujua bidhaa au huduma uliyowauzia inawasaidiaje.
2. Onesha moyo wa kuwasiadia wateja.
Ili kuweza kupata wateja wengi na kuongeza mauzo zaidi lengo kubwa la biashara yako inabidi iwe kuwasaidia watu. Bidhaa au huduma unayotoa inabidi iwe inawasaidia watu kutatua matatizo au changamoto wanazokutana nazo. Kwa mantiki hii unapofanya biashara na wateja wako hakikisha unawaeleza vizuri matumizi ya bidhaa au huduma yako na faida zake kwao. Wapatie maelezo ambayo una uhakika yatawasaidia, badala tu ya kuwauzaia na kuwaacha wakafikirie wenyewe ni jinsi gani itawasaidia.
3. Tengeneza uhaba au kuchukua hatua haraka.
Tabia moja ya binadamu ni kwamba hatupendi kupitwa na kitu. Ila pia tunapoona kitu kinapatikana wakati wowote ambao tunakitaka, shauku ya kukipata hupungua. Kwa mfano kama mteja anajua kwamba wakati wowote anaweza kupata bidhaa au huduma unayotoa anaweza asiwe na shauku kubwa. Ila kama ukitoa ofa ambayo inaisha baada ya muda mfupi wateja wako watachuku hatua ya kufanya manunuzi haraka ili wasipitwe na ofa hiyo. Hivyo toa ofa za mara kwa mara kwa wateja wako nah ii itakusaidia kuongeza mauzo.
4. Omba wateja zaidi kutoka kwa wateja wako.
Wateja wako wana ndugu, jamaa na marafiki ambao nao wanaweza kuwa wateja wako. Watumie wateja hawa kupata wateja wengi zaidi. Kwa kuwa wateja wako wameshakuamini waombe wawaambie jamaa zao kuhusu biashara yako. Wakati mwingine waombe mawasiliano ya jamaa zao hao na kisha wasiliana nao ukiwaambia kwamba jamaa yao ambaye ni mteja wako ameona wanaweza kufaidiaka na bidhaa au huduma unayotoa. Njia hii itakuongezea wateja zaidi.
5. Waridhishe wateja wako.
Pamoja na yote hayo ambayo tumejadili hapa cha muhimu kabisa ni kuwaridhisha wateja wako. Hakikisha mteja wako anaridhika kwa bidhaa au huduma uliyompatia kwa gharama alizolipia. Kwa njia hii wateja wako wataendelea kuwa na wewe kwenye biashara na watakuletea wateja wengi zaidi. Kumbuka mteja bora wa kesho kwenye biashara yako ni mteja uliyenaye leo, hivyo hakikisha unaendelea kumtunza ili uendelee kufanya nae bishara zaidi.
Ongeza mauzo zaidi ya biashara yako kwa kuongeza wateja zaidi, kuuza zaidi kwa wateja ulionao sasa na kuwatunza wateja ulionao sasa ili kuendelea kufanya nao biashara zaidi.
Nakutakia kila la kheri kwenye mafanikio ya biashara yako.
TUPO PAMOJA, TUTAKUTANA KILELENI.
asante kwa ushauri safi na unaotekelezeka.
LikeLike
Asante nawe pia kwa kusoma na utumie ushauri huo kuleta mabadiliko.
Karibu sana, TUPO PAMOJA.
LikeLike
Ni kweli Amani,mafanikio ya biashara yoyote ile ni mauzo.Njia hizi ni sahihi kabisa. Kuna njia tatu ambazo zimenigusa na nimekuwa nikizitumia na zimeniletea mabadiliko makubwa kwenye biashara yangu nazo ni 1:kujenga mahusiano mazuri na wateja.(Hapa mimi huwa nasema kila mteja ni muhimu hata anayefanya manunuzi ya shilingi 100/- 2:Kuwa na moyo wa kujali wateja. Hapa mimi nawachukulia wateja kama sehemu ya familia yangu ila kwa asilimia fulani. 3.kuridhisha wateja. Kumridhisha mteja sio tu kumpatia bidhaa aliyohitaji bali kwenda mile zaidi ya matarajio yake mfano:nyongeza kidogo,kumsikiliza kwa makini na kumfurahisha ajisikie vizuri kukutana na wewe siku hiyo. TUPO PAMOJA. BE BLESSED ALOT A FRIEND OF MINE.
LikeLike
Habari Ngutiti,
Vizuri sana kwa kuweza kutumia njia hizo na zikaleta mabadiliko makubwa kwako. Endelea kujifunza na kuongeza ubunifu kwenye biashara yako na utaona mafanikio makubwa kila siku.
Nakutakia kila la kheri na karibu sana,
TUPO PAMOJA.
LikeLike