Kuna wakati katika maisha yetu ya kila siku kutokana na kazi, mahusiano, mitazamo tuliyonayo na maisha kwa ujumla huwa ni mambo yanayotufanya tuwaze sana na hatimaye huweza kutuletea msongo wa mawazo. Hali hii ya kuwa na msongo wa kimawazo huwa haiji tu kwa bahati mbaya,  bali kuna mambo ambayo huwa yanapelekea zaidi msongo wa mawazo katika maisha yetu na kufanya maisha yetu yawe magumu kutokana na mawazo ambayo tunakuwa nayo.
Unapokuwa na msongo wa mawazo hakuna kitu ambacho kinakuwa  kinasogea katika maisha yako unakuwa ni kama vile umesimamisha maisha yako. Ni muhimu ukajua mambo yanayokufanya uingie katika msongo wa kimawazo  ili kwako iwe rahisi kuyakwepa na kuweza kuishi maisha ya amani na furaha. Kwa kupitia makala hii itakusaidia kujua chanzo cha msongo wa mawazo na kutafuta dawa. Je, unajua ni mambo gani yanaweza kusababisha msongo wa mawazo katika maisha yako? 
                
1. Kutokutimiza malengo.
Kuna wakati unaweza ukajikuta ni mtu wa mawazo na ukawa na msongo wa mawazo ndani yako ni kutokana na malengo ambayo hujaweza kuyatimiza katika maisha yako. Unaposhindwa kutimiza malengo yako na ukawa bado una nia ya kufikia ndoto zako mara nyingi kinachokutokea ni kuwa na mlimbikizo wa mawazo, unaokufanya ujiulize mara kwa mara kwa nini hujatimiza malengo yako?

2. Kukosa matumaini kwa kile unachokifanya.
Hakuna kitu kibaya katika maisha yako kama kukosa matumaini kwa kile unachokifanya. Unapokosa matumaini kwa kile unachofanya na kuona kama huwezi kufanikiwa tena katika maisha yako, usipokuwa makini utaanza kuwa na msongo wa mawazo. Hii huwa inatokea sana pale mambo yetu yanapokwenda kinyume na tulivyotarajia. Huwa tunajikuta ni watu wa kuumia sana na kushindwa kujua nini cha kufanya hali inayopelekea moja kwa moja kusongokeka kimawazo.

SOMA; Hii Ndiyo Imani Unayotakiwa Kuwa Nayo Ili Kufanikiwa.

3. Mambo yako kukuendea vibaya.
Huwa ni kitu ambacho kinatokea, mambo yetu kuna wakati yanakuwa mabaya sana ukilinganisha na miaka michache iliyopita jinsi yalivyokuwa mazuri. Wengi tunapokuwa tunalinganisha uzuri wa maisha yetu ya nyuma kidogo na uhovyo wa sasa kinachotutokea ni moja kwa moja kuwa na msongo wa mawazo. Huwa tunapatwa na msongo wa mawazo kutokana na kujiuliza maswali mengi sana ya kutaka kujua nini kinachotufanya tuteseke sasa? Wakati tulikuwa na maisha mazuri kabla?

SOMA; Vitu Muhimu Unavyotakiwa Kukumbuka Wakati Mambo Yako Yanapokwenda Vibaya.

4. Kujiona umechelewa katika maisha yako.
Hii huwa ni sababu mojawapo ambayo huwa inasababisha msongo wa mawazo kwa watu wengine.  Kujiona umechelewa katika maisha yako, huwa inatokea pale unaokuwa umejiwekea malengo yako kuwa baada ya miaka fulani lazima uwe umetimiza hili na lile katika maisha yako. Inapotokea ukashindwa kutimiza yale uliyojiwekea kulingana na jinsi ulivyokuwa umepanga hapo ndipo presha na kuvurugwa ndani ya mawazo huanza na mwisho wa siku ni lazima kitakachokutokea ni kuwa na msongo wa mawazo.

SOMA; Kama Unafikiri Umechelewa Na Umekosea Sana Katika Maisha Yako.

5. Kuingia katika mahusiano mabovu.
Unapojiingiza katika sula la mahusiano ya kimapenzi na mtu ambaye ulikuwa ukimuamini, kuwa ndio chaguo lako sahihi kwa asilimia mia moja na unapoingia kwenye ndoa mambo yakabadilika ghafla kuliko, kitakachokutokea kwako ni lazima uingiwe na msongo wa mawazo. Wengi huwa wanalia katika hili na kujikuta wakiwa hawaamini kama ni kweli yale mahusiano waliyopo ni yale waliyokuwa wakiyategemea mwanzo?Huwa ni hali inayoumiza kweli na kusababisha msongo wa mawazo. 

6. Kama hujui kile kinachokupa furaha katika maisha yako.

Katika maisha yetu huwa vipo vitu vingi tunavyovifanya kila siku. Kuna mambo tunapoyafanya huwa yanatupa furaha na hamasa ya kusonga mbele zaidi kimaisha. Katika maisha yako unapojikuta unafanya mambo mengi na ambayo hujui ni yapi yanakupa furaha ya kweli  na yepi hayakupi furaha kinachokutokea ni kusongeka kimawazo. Ni muhuimu ukajua mambo ambayo ukiyafanya yatakusaidia kukupa furaha. Usipojua utakuwa ni mtu wa kujilamisha na kujikuta wewe kuumia na kusongeka.

SOMA; Kwa Nini Ni Muhimu Sana Wewe Kuwa Na Furaha.

7. Kuwa na mitazamo hasi sana.
Kama katika maisha yako unaishi kwa mitazamo hasi sana kwa kuamini kuwa huna bahati, hujiwezi, una mikosi ama laana kama unavyoamini na mitazamo mingine hasi inayofanana na hiyo uwe na uhakika ni lazima utakuwa na msongo mawazo. Unapokuwa na mitazamo mingi sana hasi inakuwa ina nguvu ya kukuathiri wewe na kukufanya ufikiri sana vitu ambavyo vinakuumiza na kukupa msongo wa mawazo kila mara.

Kitu gani unachotakiwa kufanya ili uweze kuondokana na hali ya msongo wa mawazo?
Kwa namna moja au nyingine tayari unajua chanzo au sababu inayopelekea ama kusababisha wewe kuwa na msongo wa mawazo  katika maisha yako. Kitu pekee unachotakiwa kufanya ni kuchukua hatua za kuondokana na msongo wa mawazo ulionao. Utachukua hatua, endapo utaachana na kuwa na mitazamo hasi, kujipa matumaini kwa mipango na malengo yako na hata kufanya yale mambo yanayokupa furaha katika maisha yako.

Tunakutakia kila la kheri katika safari yako ya mafanikio makubwa na endelea kutembelea AMKA MTANZANIAkujifunza na kuboresha maisha yako kila siku.

Kwa makala nyingine nzuri hakikisha unatembelea DIRA YA MAFANIKIO kila siku kujifunza na kuhamasika.

IMANI NGWANGWALU,

0713048035/ingwangwalu@gmail.com.