Habari ndugu msomaji wa makala za JIONGEZE UFAHAMU. Ni matumaini yangu u mzima. ni mwisho wa wiki sasa, kumbuka kufanya tathmini ya mambo uliyoyafanya wiki nzima, pitia malengo yako ya wiki hii kama yote yametimia na ongeza juhudi kukamilisha mipango yako ili uweze kufikia malengo ya mwaka uliyojiwekea. Napenda nikukumbushe kuwa kila siku unayoianza ni siku ya kipekee, haitaweza kurudia tena maishani mwako, ni zawadi nzuri sana ambayo Mungu amekupa. Tumia kila siku vizuri, uwe na furaha na uguse maisha wengine pia.
Maisha ni safari. Sio mara ya kwanza kuusikia usemi huu. Naomba leo nikupe mtazamo mwingine kuhusu usemi huu.

 
Siku za hivi karibuni nilikua nasafiri safari ndefu kiasi. Safari yangu ilikuwa ni ya kutoka Kigoma kuelekea Dodoma lakini nilipanda magari yanayoenda mpaka Dar-es-salaam. Nilivyoingia kwenye gari tu saa kumi na mbili asubuhi baada ya dakika chache nilipitiwa na usingizi. Baada ya muda nilishtuka na nikaona asilimia kubwa ya abiria wakiwa wamesinzia. Baada ya mwendo mrefu sana kama masaa saba nilihisi kuchoka tena nikasinzia.
Nilipoamka kama kawaida kuna baadhi ya abiria walikua wamesinzia, wengine walikua wanasimama na kukaa ili kupunguza uchovu waliokuwa nao. Makondakta wa gari walifanya hivyo pia. Kuna wakati walikua wakirudi kwenye viti vya mwisho wa basi wanalala kidogo halafu baada ya muda wanaenda tena mbele kuongea na dereva.
SOMA; Najua Umeshasikia Hili Mara Nyingi, Sio Vibaya Ukasikia Tena Na Leo.
Safari hii ilikuwa ndefu na ilimchosha kila mmoja aliyekua ndani ya basi. Hata bila kuuliza unagundua kuwa kila mtu amechoka. Abiria wengi walikua wamekunja sura zao wakijigeuza upande huu na upande ule, hayo yote yaliashiria uchovu waliokuwa nao.
Lakini cha ajabu, wakati wote huo dereva alikua halali wala hapumziki. Nilifikiria kwa muda jinsi ambavyo dereva alivumilia. Dereva katika akili yake alikua akifikiria furaha ya kutufikisha salama kule tulikokua tunaelekea. Sisi tulipokua tunalala bado yeye hakuwaza kuhusu usingizi na kuona kama sisi tunafaidi. Kama ingekuwa hivyo angetuamsha wote ili anapokuwa akiendesha gari na sisi tusilale kama yeye ambavyo halali. Lakini basi achana na sisi abiria, hata makondakta wa gari hilo nao walikua wakipumzika. Lakini dereva hakujali kwakua alikua akifahamu lengo lake lilikua ni kuendesha gari na kutufikisha kule tunakokwenda salama. Akikutana na vikwazo ajue jinsi ya kuvikwepa bila kushauriwa na mtu yeyote pembeni, lengo kuu ni kutufikisha salama kule tuendako.
Yaani kwa kifupi dereva yeye aliangalia lengo ambalo ni kusafirisha abiria na kuwafikisha salama kule wanakoenda .
Tunajifunza nini?
Ni vizuri kuwa dereva wa gari linaloitwa maisha yako. Ukiona unasinzia, unataka upumzike, unaangalia kama wengine wamepumzika, unawalazimisha wengine wakusaidie kuendesha gari lako ambalo ni maisha yako, unategemea maoni ya wengine ili ulifikishe gari lako salama ujue kuwa upo kwenye hatari ya kusababisha ajali ya maisha yako. Kama ambavyo kuna kanuni na sheria za barabarani ndivyo ambavyo kuna kanuni mbalimbali katika maisha ya kila siku.
Dereva alikua akiongea na kondakta na mara nyingine abiria , lakini pia trafiki aliokuwa akionana nao njiani. Lakini nia yake, lengo lake lilikua ni kufika alikokua amepanga kwenda ambako alikuwa anakufahamu. Hakuna aliyeweza kumtoa nje ya kusudio lake. Pale alipokutana na vikwazo alivuka vikwazo hivyo yeye mwenyewe bila kutegemea msaada wa mtu yeyote Yule. Gari lilipoharibika, fundi alilirekebisha lakini bado yeye alibaki kuwa dereva.
SOMA; Uadilifu, Kioungo Muhimu Cha Kufikia Mafanikio.
Ni vyema kuwa imara na wenye malengo yasiyoyumbishwa kama dereva huyu. Katika safari hii ya maisha utahitaji mawazo, msaada kutoka kwa wengine, utakutana na vikwazo na mambo mengine mengi njiani. Lakini haya yote yasikutoe nje ya malengo yako uliyonayo. Hakikisha wewe ndiye unayeshikilia usukani wa maisha yako kuanzia mwanzo hadi mwisho wa safari yako ili uweze kufurahia pale unapokuwa umefikia malengo yako na sio malengo ya wengine.
Kama una swali, maoni au ushauri usisite kuwasiliana nami.
MWANDISHI: ESTHER NGULWA
MAWASILIANO: 0767 900 110 / 0714 900 110
Whatsaap: 0652 025244
Face book: ESTHER ESTHER
estherngulwa87@gmail.com