Kuna wakati tunafanya kila tunachopaswa kufanya, tunajitahidi kuhakikisha kila kitu kinakwenda sawa, na tunategemea kupata matokeo bora kwa hatua tulizochukua. Lakini kinachotokea ni tunapata matokeo ya tofauti kabisa, matokeo yanakuwa mabaya kama vile hatujafanya kitu kabisa.
Hapa ni rahisi kuanza kujilaumu na kuona kwamba tuna matatizo fulani. Tunaweza kuona tuna kisirani au bahati mbaya ndiyo maana mambo kwetu hayaendi vizuri kama kwa wengine.

Lakini huo siyo ukweli, siyo mara zote utapata matokeo yanayoendana na juhudi ulizoweka. Wakati mwingine mambo yatakwenda tofauti kabisa na juhudi ulizoweka na siyo makosa yako. Ndivyo tu dunia ilivyo, ndivyo mambo yanavyoenda.
SOMA; UKURASA WA 427; Hatua Za Kuchukua Unapokataliwa…
Lakini pia unachopaswa kujua ni kwamba, hupaswi kuacha kufanya kwa sababu umefanya mara moja na matokeo hayakuwa mazuri. Badala yake unahitaji kuendelea kufanya zaidi na zaidi, mpaka utafika wakati matokeo yatakuwa bora kabisa, yataendana na zile hatua ambazo umechukua.
Jinsi dunia inavyojiendesha sivyo sisi binadamu tunavyofikiri. Sisi tunaweza kufikiri maisha ni nipe nikupe, lakini dunia ikataka tutoe, na kutoa na kutoa tena, kabla hatujaanza kupokea.
Muhimu kabisa ni wewe kufanya kile ambacho ni sahihi, hata kama matokeo yanayokuja ni tofauti na uliyotegemea. Na kila wakati angalia ni namba gani unaweza kuboresha zaidi. Kadiri unavyoendelea kufanya yaliyo sahihi, ndivyo unavyotengeneza nafasi zaidi za kupata matokeo bora na ushindi pia.
Kila la Kheri Rafiki Yangu.
Rafiki na Kocha wako,
Dr. Makirita Amani,
Kwa kupata vitabu vya biashara na mafanikio tembelea www.kisimachamaarifa.co.tz/vitabu
Kupata blog ya kitaalamu unayoweza kuitumia kutengeneza kipato tembelea www.mtaalamu.net/patablog
“Dunia sio nipe nikupe
Kumbe wakati mwingine dunia inataka
Kutoa na kutoa nakutoa zaidi kabla ya kuanza kupokea” ASANTE SANA KOCHA.
LikeLike