3025; MIMI ni…

Rafiki yangu mpendwa,
Wakati wa sikukuu ya Pasaka, kuna jumbe nyingi ambazo watu walikuwa wanatumiana.
Mtu mmoja alinitumia ujumbe wa picha ambao ulinasa umakini wangu na kunifikirisha kwa kina.

Ujumbe huo ni kauli saba za Yesu akisema MIMI NI…
Kuna ujumbe mkubwa sana kwenye kujitamkia maneno hayo, kitu ambacho nimeona tunaweza kujifunza zaidi kwa pamoja leo.

Ni imani yangu utakuwa na mtazamo chanya wa kujifunza yale ambayo ni muhimu na kuweka pembeni swala la dini. Nimeshirikisha hapa tupate somo ambalo linamfaa kila mtu bila kujali dini yake.

Kwenye kitabu cha Yohana, Yesu ananukuliwa akitumia kauli saba za MIMI NI… (“I Am”)
Hapa nimeshirikisha kauli hizi kwa tafsiri ya moja kwa moja kutoka kwenye Biblia ya Kiingereza na siyo nukuu kutoka Biblia ya Kiswahili.

1. “Mimi ni mkate wa maisha.”
“I am the bread of life.” (John 6:35, 41, 48, 51)

2. “Mimi ni mwanga wa ulimwengu.”
“I am the light of the world.” (John 8:12)

3. “Mimi ni mlango wa kondoo.”
“I am the door of the sheep.” (John 10:7,9)

4. “Mimi ni ufufuo na maisha.”
“I am the resurrection and the life.” (John 11:25)

5. “Mimi ni mchunga kondoo mzuri.”
“I am the good shepherd.” (John 10:11, 14)

6. “Mimi ni njia, ukweli na maisha.”
“I am the way, the truth, and the life.” (John 14:6)

7. “Mimi ni mzabibu wa kweli.”
“I am the true vine.” (John 15:1, 5)


Kwa kuzisoma zinaweza kuonekana kauli za kawaida, ila ni kauli zenye nguvu kubwa sana.
Kauli hizo zimetunzwa kwa zaidi ya miaka elfu 2 na mpana leo tunazisoma, kwa sababu zina nguvu kubwa sana.

Kuna nguvu kubwa sana kwa mtu kujitamkia jambo lolote lile.
Vile tunavyokiri kwa nafsi na vinywa vyetu, ndivyo tunavyokuwa kwenye maisha ya uhalisia.

Yote ambayo Yesu alijiambia, ndiyo aliyasimamia mpaka anahukukiwa kifo.
Hakuwa tayari kutetereka kwenye kile alichoamini.
Na ndiyo maana alifanikiwa na mpaka leo tunamsoma.

Ni kauli zipi unazojinenea wewe mwenyewe na umekuwa na msimamo kiasi gani kwenye kauli hizo?
Matokeo unayoyapata kwenye maisha yanaanzia kwenye kauli tunazojinenea na msimamo tunaokuwa nao.

Kama kauli unazojiambia ni MIMI NI …. (masikini, mnyonge, wa kushindwa) na mengine mengi, na umekuwa unajiambia kauli hizo kila mara, mbele yako zitajitokeza fursa nyingi za kuhakikisha hilo linatokea.
Utaingiza kipato lakini utakitukia chote na kubaki huna kitu na hivyo kuendelea kubaki kwenye umasikini.

Rafiki, ninachotaka leo ni upindue meza, utumie nguvu ya kauli hiyo ya kujinenea na msimamo wa kujinenea ili kuyabadili sana maisha yako na kupata kweli kile unachokitaka.

Upinduaji wa meza unaanza kifikra kupitia kujitamkia na kumaanisha kweli kauli yenye nguvu ambayo ni; “MIMI NI BIASHARA YANGU NA BIASHARA YANGU NI MIMI.”
Jinenee kauli hiyo kila mara huku ukimaanisha kweli na kutekeleza kwa vitendo.
Usiruhusu kitu chochote kile kiingie kati yako wewe na biashara yako, kwa sababu nyinyi ni mapacha wa kuungana ambao hamuwezi kutenganishwa, maana mnaungana viungo vyote muhimu.

Unaweza usione nguvu ya hili kwa haraka, lakini hizi biashara tunazoona zikipata changamoto kubwa na hata kufa ni kwa sababu hazijapata umakini wa kutosha kutoka kwa wamiliki au waendeshaji wakuu wa biashara hiyo.

Unapokuwa kitu kimoja wewe na biashara yako, unaipa nguvu kubwa sana biashara hiyo kupata mafanikio makubwa.
Hata kama biashara unayofanya ni ya kuuza maji, kitu ambacho wengi wanafanya na hakuna sana cha kujitofautisha, unapoivaa biashara na biashara ikakuvaa wewe, fursa ya mafanikio inakuwa kubwa.

Japokuwa moja ya malengo yetu ni kujenga biashara ambazo zinaweza kujiendesha zenyewe bila kututegemea, bado unahitaji kuwa sana sehemu ya biashara yako wakati unajenga hilo.
Ukijaribu kujenga biashara inayojiendesha yenyewe kwa mfumo bila ya wewe kuwa biashara hiyo wakati wa ujengaji, hutaweza kulifikia lengo.

Unapojiambia kwa msisitizo na kumaanisha, MIMI NI …. unatengeneza kinga kubwa sana dhidi ya kukata tamaa pale unapokataliwa au kukatishwa tamaa.
Kama wewe ni mwanaume, halafu mtu akakuambia wewe ni mwanamke, huhangaiki kubishana naye na wala hubadiliki kuwa mwanamke kweli ili uendane na kile watu wanakuambia.
Unajijua wewe ni mwanaume na unaendelea kuishi hivyo, bila kujali nani amewahi kusema nini kuhusu wewe.

Tabia kubwa ya watu ni kuongea, hata kwenye mambo yasiyokuwa na tija wala kuwahusu kwenye maisha yao.
Kama utazingatia kila unachosikia kutoka kwa wengine, hakuna mafanikio makubwa utakayoweza kuyafikia kwenye maisha yako.

Kauli zetu 10 chanya tunazojiambia kila siku zinatumia nguvu hiyo ya MIMI NI….
Kuanzia sasa jiambie kauli hizo ukimaanisha kweli na kwenye fikra zako ukiwa na taswira halisi ya matokeo unayotaka kuyafikia.

MIMI NI … iseme kauli hiyo kwa kujivunia na kujiamini kwa hali ya juu, kisha yaendeshe maisha yako kwa kuendana na kauli hiyo.
Hilo ndiyo lenye nguvu ya kukufikisha wewe popote unapotaka kufika na kukupa chochote unachotaka kupata.

Maneno mawili yenye nguvu kubwa sana kwenye maisha yako ni MIMI NI ….
Yatumie kwa kumaanisha na msimamo ili kujenga aina ya maisha unayotaka kuwa nayo.

#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji
#BilioneaMafunzoni
#NajengaBiashara
#HakunaKingineMuhimu
#LazimaNitoboe
#NawekaKaziNifanikiwe