3082; Siyo kupanga, ni kufanya.

Rafiki yangu mpendwa,
Kwenye safari ya mafanikio, kila mtu huwa ana mipango mizuri ya jinsi ya kufikia mafanikio anayoyataka.
Lakini licha ya hilo, bado ni watu wachache sana ambao wanayapata mafanikio wanayokuwa wanayataka.

Hilo linaweza kukushangaza, iweje wengi wawe na malengo na mipango ya kufanikiwa, lakini wachache pekee ndiyo wayapate mafanikio?

Na tofauti inaanzia kwenye mahali mtu anaweka uzito.
Wale wanaofanikiwa, wakishaweka mipango, huwa wanaweka uzito kwenye kufanya. Hawapotezi muda wao kueleza na kufurahia mipango waliyonayo, kwa sababu wanajua mipango hiyo ni sehemu ndogo sana ya mafanikio.
Wanaweka muda na nguvu zao kwenye kuchukua hatua zinayowawezesha kufikia malengo na mipango yao. Na wanafanya hivyo kila siku bila kuacha.

Wale wanaoshindwa, huwa wanaweka uzito kwenye malengo na mipango yao kuliko kwenye kufanya. Huwa wanajisifia jinsi malengo yao yalivyo makubwa na mipango yao ilivyo mizuri. Wanapoteza muda mwingi kwenye kufurahia malengo na mipango yao na hata kueleza hayo kwa wengine.
Pamoja na kuwa na malengo na mipango mizuri, inapofika kwenye kuchukua hatua huwa hawafanyi hivyo kwa wakati na msimamo.
Huwa ni rahisi kuahirisha na kuacha kufanya yale waliyopanga na wala wasiumizwe na hilo.

Kitendo cha mtu kufurahia na kuridhishwa na malengo na mipango aliyonayo inakuwa kikwazo kikubwa kwake kupata mafanikio makubwa anayoyataka.
Wengi hudhani kupanga na kuwa na nia inatosha, kumbe siyo.

Pale unapokuwa na ndoto, lengo au mpango, hakuna kipimo cha nia. Kipimo halisi ni kama umefanya au hujafanya. Sababu yoyote unayojipa ya kushindwa kufanya ni kuonyesha kwamba una vipaumbele vingine zaidi ya kufanya.
Na kama una vipaumbele vingine muhimu kuliko kufanya yale uliyopanga, hakuna namna unaweza kufanikiwa.

Kama una sababu yoyote inayoweza kukuzuia usichukue hatua kwenye malengo na mipango yako, jua wazi hakuna namna utaweza kupata mafanikio makubwa unayoyataka.
Kwa sababu mafanikio makubwa ni zao la kufanya na kufanya ni kila siku.
Kuruhusu chochote kikuzuie kufanya ni kukipa nguvu ya kukuzuia usifanikiwe.

Wakati mwingine unaweza kuwa unatumia sababu za kutokufanya kukwepa maumivu yanayotokana na ufanyaji.
Sababu zinakuwa kichochoro cha kujificha kuliko kuukabili ukweli jinsi ulivyo.

Anza kupima mafanikio yako kwa ufanyaji na siyo mipango.
Weka mkazo kwenye kufanya kitu kwenye mipango yako kila siku.
Ihesabu siku yako kuwa ya mafanikio pale unapokuwa umefanyia kazi malengo na mipango yako ya mafanikio makubwa.

Acha kufurahia malengo na mipango mikubwa uliyonayo.
Usitake sifa kwenye ukubwa wa malengo na mipango, badala yake jenga sifa kwenye ufanyaji, kwa hatua unazochukua kwenye malengo na mipango uliyonayo.

Unapojieleza mbele ya wengine, usieleze sana malengo na mipango uliyonayo, bali eleza zaidi hatua ambazo tayari umeshachukua, yale ambayo umeshafanya.
Hata kama uliyofanya hayajakupa matokeo unayotaka, endelea kujieleza na kujivunia kwenye ufanyaji, kwani ukienda hivyo kwa muda mrefu, utaweza kufanya makubwa sana.

Acha kujisifia kwenye malengo na mipango mikubwa uliyonayo.
Acha kukubali visingizio unavyojipa wewe mwenyewe.
Acha kuridhika na popote ulipo sasa.
Anza kupima mafanikio yako kwa siku ambazo umefanya yale uliyopanga kufanya kwenye malengo yako ya mafanikio.
Kadiri unavyokuwa na siku nyingi ambazo umefanya kama ulivyopanga, ndivyo unavyokuwa na nafasi kubwa ya kufanikiwa.

Jivunie ufanyaji na siyo malengo na mipango.
Kila mtu anaweza kupanga, ni wachache sana wanaoweza kufanya kama walivyopanga.
Na ni wachache zaidi wanaoweza kuendelea kufanya hata pale matokeo yanapokuwa tofauti na matarajio.
Kuwa mmoja wa hao wachache sana ili uweze kupata mafanikio makubwa unayoyataka.

#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji
#BilioneaMafunzoni
#NajengaBiashara
#HakunaKingineMuhimu
#LazimaNitoboe
#NawekaKaziNifanikiwe