3088; Usielezeke kirahisi.

Rafiki yangu mpendwa,
Matokeo unayoyapata sasa kwenye maisha yako, ni zao la hatua ulizochukua huko nyuma.
Na matokeo utakayoyapata kesho, yatakuwa zao la hatua unazochukua leo.

Watu wengi huwa wanahangaika sana na matokeo wanayoyapata na kusahau hatua wanazochukua.
Matokeo yake ni kujikuta wanaendelea kupata matoke yale yale.

Kile ambacho watu wanafanya huwa kinaathiriwa sana na watu ambao wanamzunguka.
Watu hao huwa wanakuwa na madhara makubwa kwa wengine kutokana na ukaribu wanaokuwa nao na tabia yetu binadamu kufuata mkumbo.

Kitu kimoja kinachowakwamisha sana watu wengi wasipate mafanikio makubwa wanayoyataka ni tabia ya kuiga na kufuata mkumbo.
Inawezekana kitu unachoiga ni kizuri kabisa na chenye manufaa.
Lakini kama hukuweza kuwa mjanja na kuwahi kujua kitu sahihi kufanya kabla ya wengine, huwezi kupata matokeo makubwa na ya tofauti.

Unapowaiga watu wengine, hata kama unachoiga ni kizuri kiasi, unajipeleka mwenyewe kwenye uwanja wa wengine na inakuwa rahisi sana kwako kushindwa.
Kwani wale wanaokuwa wamewahi kwenye kitu hicho, kuna namna wanakuwa wamekihodhi, kiasi kwamba kila anayeiga kitu hicho, anakuwa amewanufaisha.
Hiyo ina maana kwamba pale unapoiga kitu ambacho wengine wanafanya, hata kama kina manufaa makubwa kwako, bado unakuwa umewanufaisha zaidi wale ulioiga kwao.

Njia pekee ya kuweza kuepuka kuiga na kufuata mkumbo ni kutokubali kuelezeka kirahisi.
Hiyo ina maana kwamba unafanya vitu vya tofauti na kipekee sana kiasi kwamba wengine hawaelewi unafanyaje.
Wanaweza kuona matokeo unayopata, lakini hawapaswi kuona au kuelewa ni jinsi gani matokeo hayo yamepatikana.

Usikubali kuelezeka kirahisi na wale wote wanaokuzunguka.
Kwa kufanya hivyo, hutakuwa mtu wa kuangalia na kuiga yale ambayo wengine wanafanya. Badala yake watu wanakuwa wanakazana kukujua na kuelewa kile unachofanya.
Hapo ndipo unapopata fursa ya kuwaacha nyuma wengine wasijue namna gani ya kukufikia.

Jenga aina ya biashara ambayo watu hawawezi kuielezea kwa urahisi inafanyikaje.
Lakini zalisha matokeo ambayo yana thamani kubwa kwa wengine.
Hivyo ndivyo wale wanaopata mafanikio makubwa wanavyoendesha biashara zao, kwa kutokueleweka.

Jenga biashara ambayo inaendana na maono makubwa na ya kipekee kabisa ambayo umekuwa nayo kwa maisha yako yote.
Nenda ukiendelea kuyaunda maono hayo na kuboresha biashara yako hatua kwa hatua kwa kulingana na mahitaji yaliyo mbele yako na siyo kwa kuiga wengine.
Kaa kwenye njia yako na puuza mengine yote yaliyo nje ya njia hiyo.

Acha kabisa kujihangaisha na mambo mengine mengi ambayo hayaendani na aina ya biashara unayotaka kujenga, ambayo wengine wengi hawawezi kuielezea.

Penda sana kile unachofanya kiasi kwamba hujali kingine chochote na wala hujihangaishi na yale wengine wanafanya.
Kuwa kwenye vita ya kupeleka mbele ajenda zako kuliko kuhangaika na mambo ya watu wengine.
Ni kupitia kujali zaidi mambo yako na kuyapambania ndiyo unaweza kujenga aina ya biashara ambayo haielezeki kirahisi.

Kama watu wanaweza kuelezea kwa urahisi kile unachofanya.
Kama watu wanaweza kukuiga kwa urahisi kile unachofanya.
Na kama unaiga yale ambayo wengine wanafanya.
Jua upo kwenye njia ya kujichelewesha kupata mafanikio makubwa unayoyataka.

Mafanikio makubwa hayajawahi kuwa rahisi.
Yanakutaka ujitoe kwa ukubwa na utofauti kabisa na watu wengine.
Kama unataka kwenda kwa kuiga na mazoea, jua hutaweza kuyapata mafanikio makubwa.

#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji
#BilioneaMafunzoni
#NajengaBiashara
#HakunaKingineMuhimu
#LazimaNitoboe
#NawekaKaziNifanikiwe