3263; Sababu za kuacha.

Rafiki yangu mpendwa,
Kwa chochote kikubwa unachokuwa unafanya kwenye maisha yako, ni lazima unakutana na vikwazo na changamoto mbalimbali.

Baadhi ya vikwazo na changamoto hizo vinaweza kuonekana ni vikubwa kiasi cha mtu kuona ni bora kuachana na kile anachofanya kuliko kuendelea na huo ugumu.

Kwenye maisha, kitu chochote ambacho kinakuwa rahisi kufanya, huwa kinafanywa na wengi na kinakosa thamani.
Hivyo pia ndivyo ilivyo kwenye kuacha kitu pale unapokutana na magumu, ni rahisi kuacha, wengi wanaacha na haina thamani.
Ugumu upo kwenye kuendelea licha ya magumu ambayo mtu anakutana nayo. Ni wachache wanaoweza kufanya hivyo na thamani yake ni kubwa.

Mara zote utapata sababu za kuacha chochote unachofanya, hasa pale unapokutana na ugumu. Hiyo inaonekana kuwa ndiyo njia rahisi. Lakini kama tunavyojua, rahisi inafanywa na wengi na haina thamani. Kwa maana hiyo, kuacha kile unachofanya haina manufaa kwako.

Ili upate manufaa unapaswa kufanya kile ambacho wengi hawapo tayari kufanya. Na inapokuja kwenye safari ya kufanya makubwa ni kuwa tayari kuendelea licha ya kukutana na magumu na changamoto zinazoshawishi kuacha.

Kwa kuwa sababu za kuacha ni nyingi na zinazoshawishi, unachohitaji mtu ni sababu za kuendelea kufanya licha ya magumu na changamoto unazokuwa unakabiliana nazo.
Ushindi mkubwa upo kwenye kufanya kitu kwa muda mrefu bila kuacha.
Hivyo ukiweza kujipa sababu za kuendelea licha ya yote unayokuwa unakabiliana nayo, unajihakikishia ushindi.

Hivyo pia ndivyo ilivyo kwenye kushinda na kushindwa. Sababu za kushindwa tayari unazo, sababu ambazo ukiwaambia watu watakuelewa na hata kukuonea huruma. Lakini haijalishi watu wanakuonea huruma kiasi gani, kama hujashinda ni hujashinda tu.

Unachohitaji ili kupata ushindi unaoutaka ni sababu za kwa nini unapaswa kushinda. Huwa wanasema KWA NINI kubwa inampa mtu msukumo wa kuendelea bila kukwamishwa na chochote.

Unapojikuta njia panda ya kati ya kitu kigumu kufanya na kitu rahisi, nenda njia ya ugumu. Hiyo ndiyo inayokuwa na watu wachache na hivyo ushindani wake kuwa mdogo.
Ukiweza kujipa sababu za kuendelea licha ya ushawishi mkubwa wa kuacha, utaweza kufanya makubwa sana.

Dhana hii inafaa kutumika kwenye kila eneo la maisha.
Kwenye mahusiano, mnapokutana na changamoto, huwa kunakuwa na sababu nyingi za kuvunja mahusiano hayo. Lakini hilo halisaidii, kwani hata mtu akienda kwenye mahusiano mengine, hayo hujirudia.
Anachohitaji mtu ni sababu za kuendelea kubaki kwenye mahusiano hayo na kuyaimarisha ili yasiweze kuvunjwa na chochote.

Sababu za kufanya kitu chochote rahisi huwa ni nyingi na zinazohadaa.
Mtu unahitaji kutengeneza sababu za kuendelea na magumu unayokuwa umekutana nayo.
Fanya hili na utaweza kufanya makubwa.

#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji
#BilioneaMafunzoni
#NajengaBiashara
#HakunaKingineMuhimu
#LazimaNitoboe
#NawekaKaziNifanikiwe