Habari mpenzi msomaji wa AMKA MTANZANIA? Karibu katika makala yetu ya leo ambapo leo ningependa ujiulize swali moja ambalo ni JE HAYO NDIO MAISHA YAKO HALISI? Ndugu msomaji wa makala hii kumekuwa na changamoto nyingi sana katika maisha lakini changamoto nyingine katika maisha ni zile za kujitakia. Kwa nini changamoto nyingine ni zile za kujitakia? Kwa sababu unaishi maisha ambayo siyo yako. Maisha ya kuigiza, kuangalia fulani kafanya nini na wewe ufanye kama alivyo fanya yeye. Mfano jirani yako amenunua mti wa Krismasi kwa ajili ya kusherekea sikukuu hiyo kwa sababu maisha yako ni ya kuiga kila kitu ambacho hakipo katika malengo yako na huna uhitaji nacho lakini unaona bora ununue ili usipitwe na wewe uonekane kama yeye. Je huwezi kusherekea sikukuu yako bila yakuwa na mti huo?
Ukija kushtuka utakuwa umepoteza muda, nguvu na fedha katika kuigiza maisha ambayo si yako. Kuishi maisha ambayo si yako ndio inapelekea kuingia katika madeni ambayo siyo rasmi utajikuta hufanyi cha maana utaishi juu ya kipato chako na matokeo utakuwa katika hali hiyohiyo inayokufanya usisonge mbele katika maendeleo.

KAMA UNATAKA MAISHA YA FURAHA NA MAFANIKIO, ISHI MAISHA YAKO.

 SOMA; Mambo 10 Ambayo Watu Wenye Mafanikio Huyafanya Sana Katika Maisha Yao.
Hakuna maisha ya raha hapa duniani kama kuishi maisha yako yaani unaishi maisha ambayo huna rejea yaani reference kwa mtu yoyote, unaishi katika falsafa ya maisha yako. Kama unaishi maisha yako huwezi kuishi maisha ya kuigiza hata siku moja. Watu wanapata shida mfano wakiangalia maisha ya watu wanayoishi kupitia kwenye mitandao ya kijamii jinsi watu wanavyotuma picha zao wanajikuta wanachanganyikiwa na kujiona kuwa wao hawaishi hapa duniani. Usidanganyike na maisha ya mtu anayoishi kupitia katika vyombo vya habari au mitandao ya kijamii wewe ishi maisha yako utaongeza ufanisi katika kazi, biashara na chochote kile unachofanya. Utajijengea uwezo wa kujiamini na kuishi kwa uhuru bila ya wasiwasi kuliko yule anayeishi maisha ambayo siyo yake nafsi yake ya ndani inamsuta kabisa kuwa maisha anayoishi siyo yake unajiingiza katika gharama ambazo hazina ulazima ni bora uache maisha ya kuigiza na kutumia gharama hizo ulizokuwa unaishi maisha ambayo si yako na kujiwekezea na kuweka akiba utakuwa mbali sana.
Kama unaishi kulingana na maisha yako mwenyewe huwezi kupata shida za kujitakia shida inakuja pale unapoishi maisha ya Fulani na siyo yako unakuwa kama bendera fuata upepo kule upepo unapoelekea na wewe unapelekwa tu maisha haya ya bendera fuata upepo yamewaathiri watu wengi hasa vijana kwa sasa wamekuwa wakijiingiza katika makundi mabaya kwao kama vile ya ulevi ,kucheza kamari na mengine mengi. Katika hali ya kawaida maisha ya mtu yanatengenezwa wakati wa ujana kipindi ambacho una nguvu lakini sasa vijana wengi wanajisahau na kuna msemo huu ‘’maisha yenyewe mafupi tunakula ujana ‘’
Kuishi maisha ambayo si yako huwezi kufikia mafanikio makubwa hii ni kwa sababu unaishi nje ya malengo yako, unaishi maisha ambayo siyo ya kwako unajikuta unarudi nyuma badala ya kwenda mbele kwa sababu unabeba mizigo, majukumu mengi ambayo si yako ni ya kujitakia anza leo kuishi maisha yako utapata furaha nayo furaha itakuletea mafanikio.
SOMA; Jinsi Ulivyo Unajikubali Katika Kujiletea Mafanikio Makubwa?
Kwanini watu wanaishi maisha ambayo si yao?
1. Kuishi bila ya kuwa na malengo na mipango mizuri;. Ndio katika maisha ya sasa kama huna malengo na mipango yako ni rahisi kuishi maisha kama ya bendera huna dira unapelekwa tu yaani maisha ni yako lakini huna maamuzi nayo watu ndio wanakuamulia cha kufanya ndio maana unaishi maisha ambayo si yako kila siku.
2. Kushindana; ukitaka kufanikiwa katika maisha usiishi maisha ya kushindana utaishia pabaya watu wanaishi maisha ya kushindana kila siku ndio maana wengine hawaendelei mfano jirani yako anamiliki magari zaidi ya mawili ya kutembelea na wewe una moja lakini kwa sababu unaishi maisha ya kushindana na wewe unataka kununua gari lingine bila ya kuangalia kipato chako pengine maisha yako unategemea chanzo kimoja cha mapato sasa unajikuta unaishi maisha ambayo si yako unajipatia madeni mengi kwa sababu tu ya maisha ya kushindana.
3. Sifa; watu wengine wako tayari kuigiza yaani kuishi maisha ambayo si yake ili mradi apate sifa tu sasa maisha haya ni hatari sana ya kuishi kwa sifa.
SOMA; Mambo Kumi(10) Muhimu Ambayo Kila Mhitimu Wa Elimu Ya Juu Mwaka 2015 Anatakiwa Kuyafahamu.
4. Kutojiamini; ndio muda mwingine mtu anajikuta anaishi maisha ambayo si yake kwa sababu hajiamini kama unajiamini kwa nini unaishi maisha ambayo si yako? Maisha ya kuigiza kila siku?
5. Asipitwe; kuna watu wengine wanaishi maisha ambayo kuigiza kwa sababu tu asipitwe na wakati kila mtindo mpya wa nguo ukitoka lazima anunue ili asipitwe. Maisha ya kufanya jambo ili usipitwe ni ya kujitesa sana.
Hivyo basi, tunapaswa kuishi maisha yetu na siyo kuishi maisha ya kuigiza, tathimini maisha ambayo unaishi sasa ni ya kwako na kama si ya kwako achana nayo, chukua hatua mara moja.
Makala hii imeandikwa na Deogratius Kessy ambaye ni mwandishi, mhamasishaji na mjasiriamali, unaweza kuwasiliana naye kupitia namba 0717101505 au kwa barua pepe deokessy.dk@gmail.com au unaweza kutembelea tovuti yake www.actualizeyourdream.blogspot.com