Mara nyingi uwapo katika mahusiano ya kimapenzi elewa na tambua ya kwamba, mahusiano hayo ambayo upo sasa kama hautakuwa makini  haijalishi unampenda mpenzi wako kiasi gani elewa ipo siku yatakufa.

Siombei jambo hilo litokee ila nakwambia ukweli ya kwamba kama hautakuwa makini na mahusiano yako  ni lazima mahusiano hayo yatakufa, nasema hivyo nikiwa na ushahidi wa kutosha kwa sababu wanaojenga na kubomoa mahusiano ya kimapenzi ni wapenzi wenyewe.

Na upo usemi usemao ajengaye hubomoa pia, Hata katika vitabu vya dini vinasema ya kwamba mwanamke mjinga huibomoa ndoa yake kwa mikono yake mwenyewe, si mwanamke  bali hata mwanaume naye huibomoa ndoa au mahusiano yake kwa mikono yake mwenyewe.

Unajua ni sababu zipi ambazo hufanya mahusiano  mengi yafe. Kama hujui  sababu kubwa ni :

Kumlinganisha mpenzi wako na mtu mwingine.

4d1bd-maadui2bwa2bmahusianoHii nayo ni tabia mbaya katika tabia mbaya ambazo unazijua au ulizowahi kusikia. Hii ni kwa sababu katika mahusiano mengi wapo watu wanatabia za kuwalinganisha wapenzi wao na wapenzi wao wa zamani.

Unakuta mtu anasema ya kwamba wanaume au wanawake wote ni sawa, kauli kama hizi si nzuri katika mahusiano, mtu mmoja kukutenda katika mahusihano kusikufanye akawafananisha wanaume au wanawake wote ya kwamba wote ni walewale.

SOMA; Makosa Mawili (02) Makubwa Yanayogharimu Maisha Ya Watu Wengi.

Katika mahusiano yako epuka kumfananisha mpenzi wako na watu wengine ambao ulishawahi kuwa nao na mahusiano, jifunze kutamka maneno yenye faraja na yenye kuamsha hisia mpya za kimapenzi.

Hisia hizi hujengwa kwa upendo wa kweli mathalani maneno yenye kutia moyo na kufanya mpenzi wako ajione yeye ni wa thamani kupendwa na wewe. Mwanaume au mwanamke hupenda zaidi ukimwambia ‘hakuna mwanaume/ mwanamke mwingine wa kufanana na wewe.’

Maneno kama haya wengi huyaona ni madogo na labda hayana thamani yeyote, ila ninachotaka kukwambia maneno kama haya yana nguvu sana ya kujenga msisimko mpya wa mapenzi. Hivyo kama unataka kudumu katika mahusiano kwanza jifunze kutomlinganisha mpenzi wako na mtu mwingine lakini pili jifunze kumwambia mpenzi wako maneno ambayo yatajenga mahusiano yenu na si kubomoa.

Pia tafiti zinaonesha mwanaume anapenda kuhakikishiwa kwamba hakuna mwanaume mwingine kama yeye. Yeye ndiye mzuri au bora kuliko wanaume wengine hivyo mwanamke anapoanza kuonesha tabia za kumlimnganisha na mwanaume mwingine linakuwa tatizo kubwa.

Wanawake wanapaswa kuwa makini katika eneo hilo. Hata kama umeona kuna kitu kizuri kimekuvutia kutoka kwa mwanaume mwingine, kamwe usije kumwambia mwenzi wako. Baki nalo moyoni. Jipe moyo kwamba mwanaume uliyenaye ndiye bora kuliko wanaume wote duniani.

Si kwa mwanamke tu bali hata kwa mwanaume iwe hivyo hivyo pia, hakuna jambo zuri kama suala ambalo litawafanya muishi vizuri katika mahusiano yenu ya kimapenzi  mpaka kifo kitakapowatenganisha.

Mpaka kufikia hapo sina la ziada ujumbe wangu kwako acha mara moja kumlinganisha mpenzi wako na mtu mwingine, jifunze kumuona yeye ni wa pekee  sana kuliko watu wengine ambao unawaona katika macho yako.

Makala hii imeandikwa na Afisa MIpango wa Mafanikio,

Benson Chonya,

http://www.amkamtanzania.com,

0757-909942.