3061; Kuaminiana.

Rafiki yangu mpendwa,
Dunia inaendeshwa kwa msingi mkuu wa kuaminiana.
Bila ya kuaminiana, dunia haiwezi kwenda.

Tunaweza kufanya yote tunayoyafanya kwenye maisha, kwa sababu tunaweza kuwaamini wengine bila hata ya sababu yoyote.

Tunakuwa tayari kuyaweka maisha yetu kwenye hatari kubwa kwa kuwaamini wengine kwamba watafanya kile kilicho sahihi.

Fikiria unaenda kwa daktari, ambaye humjui wala hakujui, lakini unaamini atakupa matibabu sahihi kwa yale yanayokusumbua, na mara nyingi ndivyo inavyotokea.

Fikiria pia unaendesha gari barabarani na kuna madereva wengine nao wanaendesha magari, huwajui na hawakujui, lakini unaamini watafuata sheria za barabarani na kuepuka kusababisha ajali.

Au unapanda kwenye gari ambalo dereva humjui wala yeye hakujui, lakini unaamini ataendesha kwa usalama na kufika safari yako salama.

Au pia unakwenda kwenye hoteli ambapo mpishi humjui wala hakujui, lakini unakuwa tayari kula chakula kwa kuamini kimeandaliwa vyema na hakitakuwa na madhara kwako.

Hivyo ndivyo dunia inavyoendeshwa, kwa kuaminiana, bila hata ya kuwa na sababu au uthibitisho wowote.
Na mara nyingi kuaminiana huko kumekuwa sahihi na kurahisisha mambo mengi.

Japo huwa kuna watu wanatumia vibaya kuaminiana huko na kuishia kuleta madhara kwa wengine.
Hapa ni pale wale wanaotaka kujinufaisha bila kujali wengine wanapotumia mfumo huu wa kuaminiana kupata yale wanayotaka kupitia kuwaumiza wengine.

Watu hao wachache wanaotumia vibaya mfumo huu wa kuaminiana wamesababisha watu wengi kuwa na mashaka juu ya mfumo huo wa kuaminiana.
Kuna watu mpaka wameamua kwamba hawawezi kumwamini mtu yeyote.
Lakini hiyo ni kujiambia tu, huwezi kuyaendesha maisha yako bila kumwamini mtu yeyote.
Kuna vitu vingine hata kama huna uhakika, inabidi uamini tu ili kurahisisha maisha.

Inapokuja kwenye safari ya mafanikio, uaminifu ndiyo kitu ambacho kinahitajika kwa wingi na uhakika sana.
Safari ya mafanikio inahusisha fedha na nafasi nyeti, vitu ambavyo kila mtu anavitaka, lakini wengi hawapo tayari kuvifanyia kazi.
Hilo linawafanya wawe tayari kutumia njia zisizo za uaminifu kujinufaisha na fursa hizo.

Hilo limewafanya watu wengi waliopo kwenye safari ya mafanikio kuwa na tahadhari kubwa sana, wengi wakisema wazi hawawezi kumwamini mtu yeyote.
Na wanaweza kuwa sahihi sana, ukizingatia maumivu ambayo walishakutana nayo na jinsi ambavyo watu wanataka mafanikio kwa tamaa.

Lakini pia, hakuna namna mtu utaweza kufikia mafanikio makubwa kama humwamini mtu yeyote.
Kuna hatua inafika inabidi tu uwaamini baadhi ya watu bila ya uthibitisho wowote ule.
Inakubidi ufanye hivyo ili mambo yaweze kwenda.
Kwani ukisema ni mpaka uthibitishe kile kitu peke yako, hutaweza kukamilisha mengi yanayokusubiri.

Lakini hilo haliondoi hatari iliyopo kwa baadhi ya watu kutumia vibaya mfumo huo wa kuaminiana, kwa kujinufaisha binafsi na kuwaumiza wengine.

Jinsi ya kukabiliana na hilo ni kutumia kanuni maarufu ya kukabiliana na watu usiowajua. Kwanza unaanza kwa diplomasia, halafu unaangalia watajibuje, kisha kinachofuata ni kuwajibu kwa jinsi walivyokujibu.
Wakikujibu kwa diplomasia unaendeleza diplomasia. Na wakikujibu kwa jeuri unaendeleza jeuri.

Kwa kila unayekutana naye au kuhitaji kushirikiana naye kwenye safari ya mafanikio, anza kwa kumwamini.
Halafu kadiri mnavyokwenda, utamchukulia vile atakavyokuwa.
Kama atakuwa mwaminifu basi utaendelea kumwamini.
Na kama hatakuwa mwaminifu basi unaacha kumwamini.

Hii inarahisisha sana kuchagua watu wa kushirikiana nao.
Huhitaji kutumia nguvu nyingi awali, unachagua yeyote anayeonyesha nia njema, unamwamini na kuanza naye, kisha kuangalia vile mnavyokwenda.
Akiwa mwaminifu unaendelea kumwamini bila ya shaka.
Lakini pale unapomkamata na kitendo chochote cha kukosa uaminifu, huwi tena na sababu ya kuendelea kumwamini, hata ajitetee vipi.
Kama ushahidi wa kukosa uaminifu upo, mtu huyo siyo mwaminifu na hupaswi kuendelea kumwamini.

Kwa kutumia kanuni hii, inaturahisishia sana kufanya maamuzi.
Tuangalie eneo moja ambalo limekuwa na changamoto sana kwenye kupata watu sahihi, eneo ambalo ni kuajiri.
Wakati unawasaili watu kwa ajili ya kuajiri wanaahidi vitu vingi sana.
Lakini wengi ukishawaajiri hawawezi kutekeleza.
Hilo linaweza kukufanya usiwaamini watu na hatimaye kuacha kuajiri kabisa.
Lakini huwezi kukuza biashara yako bila ya kuwa na wafanyakazi.
Ni lazima uwaamini watu na kuwaajiri hata bila ya kuwa na uthibitisho.

Kwa kutumia kanuni hii tuliyojifunza hapa, unapowafanyia watu usaili na wakawepo ambao umeshawishika wataweza kazi na ukawaajiri, basi anza kwa kuwaamini.
Amini watayatekeleza majukumu yao vizuri kama walivyoonyesha kwenye usaili.
Wafundishe vizuri kabisa jinsi ya kutekeleza majukumu yao.
Wasaidie kwa kila namna kuhakikisha wanafanikiwa kwenye kutekeleza majukumu yao.
Halafu waangalie jinsi wanavyofanya.
Kama watafanya vitu ambavyo ni vya kukosa uaminifu, wamekupa sababu ya kutokuwaamini.
Wakishaonyesha ushahidi kwamba wamekosa uaminifu, huna tena sababu ya kuendelea kuwaamini na hapo utaachana nao au kuwaondoa kwenye nafasi ambazo kukosa kwao uaminifu kutakudhuru.

Kama unajiambia huwezi kumwamini mtu yeyote yule bila ya kuthibitisha mwenyewe, maisha yako yatakuwa magumu sana, utazikosa fursa nyingi.
Mtu akishakupa sababu ya kutokumwamini, ni tatizo binafsi kwako kama utaendelea kumwamini na akakuumiza.
Hii ni kanuni rahisi ambayo itakusaidia kwenye mengi.

Hii ni kanuni ambayo nimekuwa naitumia kwa watu wote ninaojihusisha nao na imenirahisishia sana.
Awali kwenye safari yangu ya maisha, baada ya kuwa naangushwa na baadhi ya watu niliowaamini nilikuwa na msimamo wa kutokukwamini mtu yeyote yule mpaka nithibitishe mwenyewe.
Lakini hilo likawa ukomo mkubwa sana kwangu kukua, hasa kupitia kushirikiana na watu wengine.

Ni mpaka pale nilipojifunza kanuni hii kupitia nadharia ya mahusiano inayoitwa Game Theory.
Hapo ndipo nilipojifunza kumwamini kila mtu hata kama sina uthibitisho, halafu kuamua kuendelea kumwamini kulingana na matokeo anayotoa yeye mwenyewe.
Kama mtu atanipa sababu ya kuendelea kumwamini, nitaendelea kumwamini.
Lakini kama atanipa sababu za kutokuendelea kumwamini, kama atakosa uaminifu kwa ushahidi wa wazi kabisa, siendelei tena kumwamini.

Kwa kanuni hiyo nimeweza kuwafikia wengi, kuachana na wengi na kubaki na wachache ambao kweli wamestahili kuaminiwa.
Na hivyo ndivyo nitakavyoendelea kwenda.

Ndivyo pia tunavyojenga programu zetu za KISIMA CHA MAARIFA na BILIONEA MAFUNZONI.
Namwamini kila anayehitaji huduma hizi, lakini ili waendelee kuzipata, lazima niendelee kuwaamini.
Kama mtu atanipa sababu ya kutokumwamini, hapo unakuwa mwisho wake wa kupata huduma hizi.
Haijalishi nimekuwa na mtu huyo kwa muda gani, kama ushahidi upo wazi kwamba amekosa uaminifu, mambo yanaishia hapo.

Uaminifu ni kitu kikubwa na muhimu sana ambacho mtu anapaswa kukilinda sana.
Hakunaga bahati mbaya kwenye kuvunja uaminifu, inakuwa ni kujidhihirisha kwa kile ambacho kilikuwa kinaendelea kwa kificho.
Ubaya wa kukosa uaminifu ni kitu ambacho huwezi kwenda nacho kwa kificho kwa muda mrefu, mambo yatajidhihirisha tu.
Hivyo kama unataka uaminike bila ya shaka, mara zote kuwa mwaminifu, kwenye mambo makubwa na mambo madogo.

Hivyo ndivyo ninavyokwenda na wewe, nakuamini mpaka pale utakaponipa sababu za kutokukuamini tena.
Hivyo pia ndivyo ninavyokushauri uende na mimi, niamini mpaka pale nitakapokupa sababu za kutokuniamini.
Kwa njia hiyo tutapunguza mkwamo usio na maana.

#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji
#BilioneaMafunzoni
#NajengaBiashara
#HakunaKingineMuhimu
#LazimaNitoboe
#NawekaKaziNifanikiwe