3125; Tengeneza bahati yako mwenyewe.

Rafiki yangu mpendwa,
Umewahi kukutana na mtu ambaye amepata mafanikio makubwa ambayo kwa uwezo wake siyo kitu cha kutegemewa?
Jibu litakuwa ni ndiyo na huwa tunapokutana na watu wa aina hii, moja kwa moja tunajiambia wana bahati.

Au hata huenda ni wewe mwenyewe, kuna hatua ambazo umepiga na watu wengine wanaona una bahati.

Bahati ni kile kinachoonekana kwa haraka kwa nje, hasa pale watu wanapokosa maelezo ya nini kimeendelea kwa ndani.
Hivyo basi ni kitu ambacho kila mtu anaweza kukitengeneza kwa ndani, kama atajua yale yanayohitajika.

Ili uweze kutengeneza bahati yako mwenyewe, kuna vitu vitano unavyopaswa kuvizingatia.

Kitu cha kwanza ni kuwa na ujuzi na uwezo wa kufanya vizuri kile unachofanya.
Huwezi kujenga bahati kama unafanya kwa kubahatisha.

Kitu cha pili ni kuweka juhudi kubwa kwenye kufanya kile unachofanya.
Juhudi zinahitajika sana ili kukusogezea bahati yako karibu.

Kitu cha tatu ni msimamo mkali kwenye kuweka juhudi kwa uendelevu bila kuacha.
Hakuna kitu utakachofanya mara moja na ukawa umemaliza. Lazima urudie rudie kufanya kwa muda mrefu bila kuchoka.

Kitu cha nne ni kuweza kutegemewa, pale unapoahidi kitu unatimiza kama ulivyoahidi. Utaratibu wowote ulionao unakuwa endelevu kiasi kwamba mtu anaweza kukutegemea bila ya shaka yoyote.

Kitu cha tano ni kuwa na shauku kubwa kwenye kile unachofanya na maisha kwa ujumla.
Shauku yako inawavuta watu kuja kwako kitu ambacho kitakuletea bahati nyingi ambazo wengine hawawezi kuzipata.

Vitu hivyo vitano lazima viende kwa pamoja ili bahati iweze kutengenezeka kwa uhakika.

Kuwa na ujuzi wa kile unachofanya peke yake haitoshi, ni lazima pia uweze kutegemewa kwa hicho unachofanya na pia uwe na shauku kubwa kwenye kukifanya.

Juhudi kubwa unazoweka kwenye kile unachofanya zitakusaidia sana ndani ya muda mfupi. Msimamo mkali unaokuwa nao kwenye ufanyaji unakusaidia sana kwa muda mrefu.

Unapofanya haya matano mara zote na kwa mwendelezo unakuwa umejipa ufunguo mkuu ambao unaweza kufungua kila aina ya mlango.
Hakuna kitakachoshindikana kwako kama mara zote utaegemea kwenye mambo haya matano.

Uzuri haya ni mambo ambayo yapo ndani ya uwezo wako na unaweza kuamua kuanza kuyafanyia kazi mara moja na kwa mwendelezo.
Amua sasa na yafanye kuwa sehemu ya maisha yako yaliyobakia hapa duniani.
Utashangaa jinsi ambavyo utakaribisha fursa nzuri na kubwa kwako, kitu ambacho kwa wengine utaonekana mtu mwenye bahati sana.
Ambacho hawatajua ni jinsi ambavyo umekazana kujenga bahati yako wewe mwenyewe.

Kila mtu anaweza kujenga bahati yake yeye mwenyewe, lakini wengi hawafanyi hivyo kwa sababu wanapenda kwenda na mazoea badala ya kujisukuma kwa utofauti.
Wewe kuwa tofauti na utaweza kufanya makubwa kwenye maisha yako, kwa kuzingatia haya matano uliyojifunza hapa.

#NidhamuUadilifuKujituma
#AfyaUtajiriHekima
#KaziUpendoHuduma
#UpekeeUdadisiUbunifu
#UshirikianoUtegemeanoUwajibikaji
#BilioneaMafunzoni
#NajengaBiashara
#HakunaKingineMuhimu
#LazimaNitoboe
#NawekaKaziNifanikiwe