Sikiliza hapa;

Rafiki yangu Mpendwa,

Mipango siyo matumizi. Tunaweka vizuri malengo na mipango ya kile tunachokuwa tunataka. Na kuanza kufanyia kazi yale tunayokuwa tumeyapanga. Lakini matokeo tunayoyapata, yanakuwa ni tofauti kabisa na matarajio tunayokuwa nayo.

Hapo ndipo safari ya watu wengi inapoishia. Kwa sababu wamefanya kile walichopaswa kufanya na matokeo hayajaja, wanakimbilia kwenye kitu kingine kinachoonekana kuweza kuleta matokeo kwa urahisi zaidi. Lakini hata kwenye kitu hicho kingine, mambo yanajirudia hivyo hivyo.

Kuna sababu nyingi sana ambazo watu wamekuwa wanatoa kama kikwazo kwao kufanikiwa. Nyingi ni sababu nzuri na zinazowapa watu faraja ya kwamba tatizo siyo wao, bali watu wengine au hali zilizopo.

Lakini tunapochunguza kwa ndani, ukweli unakuwa ni tofauti kabisa. Tunaona wazi kwamba kitu cha kwanza kinachosababisha watu kushindwa ni kutokuweka jitihada za kutosha. Ndiyo, wengi wanajaribu, lakini ni kwa jitihada za kawaida. Na pale matokeo yanapokuwa siyo mazuri, safari inakuwa imeishia hapo.

Kwenye barua hii tunaenda kuvunja hayo mazoea mabaya, ambayo yamekuwa kikwazo kikubwa kwetu. Tunaenda kujenga mpango mpya wa kuweka juhudi zaidi kwenye kila tunachopanga ili tuweze kupata mafanikio makubwa tunayoyataka.

1. Haupo Tena Shuleni.

Kuna mambo ya kitoto tulikuwa tunayafanya tulipokuwa shuleni, lakini cha kushangaza tunaendelea nayo kwenye maisha. Tunasahau kwamba hatupo tena shuleni, na hatujiandai tena kuishi, kwani kila siku ni maisha yaliyokamilika.

Moja ya mambo hayo ni kuamini wanafunzi wenye akili hawasomi sana, ila wanafaulu. Na hilo linafanya wale wanaoonekana wanasoma sana basi hawana akili. Hilo lilifanya wengi kupuuza kuweka juhudi kubwa kwenye masomo, kwa kuona ni kuonyesha huna akili.

Kitu kingine kilichotokea ni watu kutokuweka juhudi kubwa sana kwenye masomo, halafu pale matokeo yanapokuja ambayo siyo mazuri, wanajifariji kwamba kama wangeweka juhudi zaidi, basi wangefaulu zaidi. Yaani ni kama mtu anajiambia; ‘Si unaona, sijasoma sana lakini nimepata alama B, kama ningesoma sana kama wengine, lazima ningepata alama A.’

Kwa njia hiyo, watu wanaacha kuweka juhudi zaidi, ili kupata sababu ya kuhalalisha matokeo ya chini wanayoyapata. Kitu ambacho watu wameendelea nacho mpaka kwenye utu uzima.

Unakuta mtu anafanya kitu kwa viwango vya chini, na anapata matokeo ya chini, kisha anajifariji kama angefanya kwa viwango vya juu, basi angepata matokeo ya juu. Sasa ya nini ujifariji? Kwa nini usifanye kwa viwango vya juu kweli ili upate hayo matokeo ya juu?

Unasema biashara yako haina mtaji mkubwa, au haina wafanyakazi wazuri, au haina wateja wengi ila bado inaweza kwenda, nini kinachokuzuia kufanya hayo yote ili upate matokeo makubwa zaidi?

Unajisifia huwezi muda mwingi kwenye kazi au biashara yako kama wengine, lakini unapata matokeo kama wanayopata wao. Kwa hiyo? Nini ambacho kinakuzuia kuweka juhudi kama zao ili upate matokeo makubwa kuliko yao?

Umefika wakati sasa wa kuachana na mambo ya shule, kwa kutaka sifa zisizokuwa na tija. Kinachoangaliwa ni ushindi, matokeo unayoyapata. Kama umepata matokeo ya chini, hata kama utawaambia watu kwamba hukuweka juhudi zaidi, haibadili hali kwamba hujapata matokeo.

Wajibika kama mtu mzima, weka jitihada kubwa zaidi kwenye kila unachofanya ili upate matokeo makubwa. Na kama utaweka jitihada na usipate matokeo makubwa, hakuna tatizo lolote. Kwa sababu utahitajika kuweka jitihada kubwa zaidi ya ulizoweka awali.

Yaani, unafanya kwa ukubwa na ukishindwa unafanya kwa ukubwa zaidi. Na unarudia hilo mpaka upate kile unachotaka.

Kwenye #BaruaYaKocha nimekupa sababu nyingine nne za kuweka jitihada zaidi kwenye chochote unachofanya ili upate mafanikio makubwa. Kitu kimoja zaidi ni kuna jaribio ambalo nimekupa, ambalo ukilifanya utajionea matokeo mwenyewe.

Soma barua hiyo hapa; #BZK067; Vipi Kama Ungeongeza Jitihada Zaidi?