Pamoja na umuhimu mkubwa wa kujiwekea malengo kwenye maisha tuliozungumzia kwenye makala zilizopita(kama hujazisoma bonyeza hapa), bado kuna watu ambao hawajajishughulisha kujiwekea malengo.
Unaweza kuwa umesoma kuhusu kuweka malengo ila bado unaona hakuna haja ya kuweka malengo kwa sababu maisha bado yanaenda bila hata ya kuweka na kuandika malengo. Unaona kuweka malengo ni kitu cha kawaida sana ambacho hakiwezi kuyabadili maisha yako na hivyo hujajisumbua kukaa chini na kuandika ni vitu gani unataka kwenye maisha ama unataka maisha yako yaweje.
Unaweza kuwa unafikiria hivyo kwa sababu hujajua hasara kubwa unayoipata kwa kutokuweka malengo kwenye maisha yako. Hujajua mpaka sasa ni kiasi gani umepoteza kwa kutokuwa na mpango makini na maisha yako. Unaweza kuona maisha yanakwenda bila ya kuwa na malengo ila hayo sio maisha unayostahili. Kuna maisha bora zaidi ya hayo kama utajua ni nini unafanya kwenye maisha.
Kama huna malengo na maisha yako maana yake ni kwamba huna mpango na misha yako. Na kama huna mpango na maisha yako hii ndio hasara kubwa unayoipata;
KAMA HUNA MPANGO NA MAISHA YAKO WATU WATAKUTUMIA KWENYE MIPANGO YA MAISHA YAO.
Kwa kuwa wewe umegoma kuweka mipango ya maisha yako, walioweka mipango watakutumia wewe kufikia malengo yao. Unajisikiaje pale unapogundua ya kwamba unatumika kutekeleza mipango ya mtu mwingine? Hii ni hasara kubwa na udhalilishaji wa utu na maisha yako.
Huweki malengo ya kujiajiri mwenyewe ama kufanya biashara, watu wanakutumia kwa kukuajiri.
Huweki malengo ya kuwa na afya bora, watu wanatumia mwili wako kupata fedha pale unapokuwa na afya mbovu.
Huweki malengo ya kuyasimamia na kuyaboresha maisha yako, watu wanakutumia kwa kukudanganya kwamba watayaboresha maisha yako.
Hivyo ndivyo maisha yalivyo, huna mpango na maisha yako unatumika kwenye mipango ya wenzako.
Kama bado unatumika na umeshachoka kutumika unaweza kuondokana na hali hiyo kwa kuanza sasa kwa kujiwekea malengo. Sio kazi ngumu kujiwekea malengo, na kama huna uhakika ni jinsi gani unaweza kuweka malengo utakayofikia soma; jinsi ya kuweka malengo utakayofikia.
Tarehe 18/01/2014 itafanyika semina ya kuweka malengo na kubadili maisha dar es salaam. Kama bado unashindwa kuweka malengo na kuyafikia, utajifunza kwenye semina hii. Pia utajifunza jinsi ya kuchukua hatua juu ya maisha yako na uwe na maisha bora. Kama utahitaji kuhudhuria semina hii tafadhali bonyeza maandishi haya kisha ujaze fomu fupi itakayotokea. Ufanye mwaka 2014 kuwa mwaka wa mabadiliko makubwa kwenye maisha yako, anza kwa kuhudhuria semina hii.