Kuna njia rahisi sana ambayo watu huitumia kujiona wao ni bora zaidi ya wengine.
Pamoja na urahisi wake, njia hii ni ya hovyo sana kwani hata inapowafanya wajione wao ni bora bado kiuhalisia wanakuwa sio bora, hasa ndani yao wenyewe, na wanalijua hilo.
Njia hii rahisi ya wewe kujiona uko bora ni kuwafanya wengine waonekane wako hovyo zaidi yako, kuwadhoofisha. Na hii haiishii tu kwenye kufikiri kwamba hawa hawako bora, bali unahakikisha unawafanya wajione hawako bora, kwa kuwaambia au kwa jinsi unavyokuwa unawafanyia.
Watu wengi wamenasa kwenye mtego huu, wa kuhakikisha kila anayeonekana yuko bora basi wanatafuta njia ya kumfanya asionekane bora. Kutafuta njia za kumrudisha nyuma, za kumfanya ajione yeye bado ni wa chini kuliko wao.
Njia hii inaweza kufanikiwa kwa juu juu, yule ambaye uliona anakuwa bora kuliko wewe anarudi chini. Lakini kitu kibaya sana ni kwamba kumshusha mwingine chini hakukupandishi wewe juu. Kunakufanya uendelee kuwa chini, ili uwashikilie chini wale uliowashusha.
Ufanye nini?
Usitafute njia ya mkato ya kuwa bora. Ubora unatokana na wewe mwenyewe, kwa maisha unayochagua kuishi na kwa jinsi unavyochagua kufanya shughuli zako. Ubora unatokana na juhudi zako wewe binafsi, na ubora au kutokuwa bora kwa wengine sio jukumu lako.
Unapoona wengine wanakuwa bora zaidi, watakie wema, furahia ubora wao huo kwa sababu unafungua njia kwa wengi. Unawafanya wengi waone kumbe inawezekana na wao kulenga kuwa bora zaidi. Lakini kama utakazana kuwashusha chini, unawazuia na wengine wengi na wao kupanda.
Kuwashusha wengine ili wewe uonekane uko juu inaweza kuonekana ni vizuri kwa muda mfupi, lakini hii itakuzuia kufika mbali kwa muda mrefu.
SOMA; Hii Ndio Sababu Kwa Nini Watu Wanafurahia Pale Unapoanguka…
TAMKO LANGU;
Nimejua kuwarudisha wengine chini au kuwazuia wasionekane bora zaidi yangu hainifanyi mimi kuwa bora. Ubora wangu unatokana na uchaguzi wangu na juhudi ninazoweka. Kuanzia sasa nitawatakia kheri wale wote wanaokuwa bora kwa sababu kwa njia hii mimi na jamii nzima tutajifunza mengi zaidi.
NENO LA LEO.
Criticism and pessimism destroy families, undermine institutions of all kinds, defeat nearly everyone, and spread a shroud of gloom over entire nations.
Gordon B. Hinckley
Kukosoa na mtizamo hasi kunaharibu familia, kunadhoofisha taasisi za kila aina, kumwangusha karibu kila mtu na kusambaza giza kwenye taifa zima.
Kumdhoofisha anayeonekana kuwa bora kuliko wewe, hakukufanyi wewe kuwa bora zaidi.
Rafiki na Kocha Wako,
Makirita Amani,
makirita@kisimachamaarifa.co.tz
TUPO PAMOJA.