Mwanafalsafa Aristotle alisema kuna aina tatu za urafiki.

Moja ni urafiki wa matumizi, hapa watu wanakuwa marafiki kwa sababu kuna kitu ambacho kila mmoja ananufaika nacho kwa mwingine, yaani kila mmoja anamhitaji mwingine kwenye kile anachofanya. Mfano mzuri ni urafiki kwenye kazi au biashara, ambapo watu wanakuwa marafiki kwa sababu wanafanya kazi au biashara pamoja. Uhitaji uliopo unapoisha, urafiki huu hukoma.

Mbili ni urafiki wa raha, au kama wengi wanavyopenda kuita, urafiki wa bata. Huu ni ule urafiki ambapo watu hukutana pamoja kwa ajili ya starehe na burudani mbalimbali. Urafiki huu upo wakati wa raha tu, nje ya hapo urafiki huu hukoma.

Tatu ni urafiki wa wema au urafiki wa kweli, huu ni ule urafiki wa nyakati zote, urafiki ambao hauna sababu nyingine nyuma yake. Hapa watu wanakuwa marafiki kwa sababu kila mmoja anampenda na kumjali mwingine, na siyo kwa sababu nyingine yoyote. Urafiki huu hudumu nyakati zote.

Wengi wamekuwa wakilalamika kwamba hawapati marafiki wa kweli, lakini wanachoshindwa kujua ni aina gani ya marafiki ambao wanao. Kama ulikuwa unafanya kazi eneo fulani na ukawa na marafiki hapo, kisha ukaacha kazi eneo hilo na ukapoteza marafiki hao, hakuna ubaya, kilichowaleta pamoja kimeondoka hivyo urafiki huo unakoma.

Kadhalika kama kuna wakati ulikuwa na fedha nyingi na ukawa mtu wa starehe, hapo ukawa na marafiki wengi, lakini fedha hizo zikaisha na marafiki hao wakakukimbia, hakuna tatizo, kilichowaleta kwako hakipo tena, hivyo hawana sababu ya kuendelea kuwa na urafiki na wewe.

Unapojua aina ya urafiki ulionao, inakupunguzia kujiumiza pale urafiki huo unapoisha.

Urafiki wa kweli huwa unapimwa kwenye nyakati ambazo ni ngumu, hapo ndipo unaweza kujua nani rafiki wa kweli na nani ni rafiki wa maslahi au starehe. Hivyo unapopitia magumu, jifunze mengi, ikiwepo pia marafiki wa kweli kwako.

Kwa kumalizia, kumbuka kwamba urafiki wa kweli haulazimishwi, ni kitu ambacho kinakuja kwa asili kwa sababu watu wawili wamejikuta wakiweza kwenda pamoja na kujaliana. Ukiona unalazimisha urafiki, jua kuna kitu hakipo sawa, na hata kama utafanikiwa kuulazimisha, urafiki huo utaanguka pale mambo yatakapokuwa magumu kwa mmoja wenu.

Kila la Kheri Rafiki Yangu.

Rafiki na Kocha wako,

Dr. Makirita Amani,

www.amkamtanzania.com/kocha