Kama ambavyo mwanafalsafa Seneca amewahi kuandika, tatizo la muda siyo kwamba ni wa uhaba na hautoshi, bali ni mwingi na tunautawanya hovyo.
Ndiyo maana swali maarufu la kujiuliza kama leo ingekuwa siku yako ya mwisho hapa duniani ungefanya nini, linatusaidia sana kuweka vipaumbele vyetu sawa. Tunapojua kwamba bado tuna muda, huwa tunatumia muda tulionao vibaya. Kwa kujiambia kuna kesho, unaipoteza leo na kuahirisha ambayo yangeweza kufanyika leo.
Hivyo pia ndivyo ilivyo kwenye kazi, unapokuwa na muda mwingi wa kufanya kazi, unapoteza sehemu kubwa ya muda huo. Ndiyo maana kazi zenye ukomo wa muda, ukomo unapokaribia ndiyo wengi hufanya.
Kama unataka kutumia muda wako wa kazi vizuri, panga majukumu yako kwa muda mfupi kuliko ulivyozoea. Jiulize kama ungekuwa na saa moja pekee ya kufanya kazi kwenye siku yako, je ungefanyaje kazi ulizonazo sasa.
Na ukweli ni kwamba, muda ulionao wa kuweka umakini wako kwenye kazi bila ya kusumbuliwa na chochote, hauzidi saa moja, hasa kwa zama tunazoishi sasa. Hivyo tenga saa hiyo moja na chagua jukumu ambalo ni muhimu, ambalo ukilikamilisha litasaidia sana kwenye majukumu mengine.
Kila siku tenga saa moja ya kazi, ambapo hakuna usumbufu kabisa, saa ambayo hutaruhusu chochote kikuingilie, kisha weka umakini wako wote kwenye kile unachofanya.
Katika majukumu unayotekeleza kila siku, jiulize ni jukumu lipi ukilipa saa yako moja kwa ukamilifu litakuwa na matokeo yatakayosaidia zaidi kwenye majukumu mengine. Ukishajua jukumu hilo, lifanyie kazi.
Kulingana na kazi zako au mazingira yako, unaweza kutenga muda tofauti, labda masaa mawili, matatu na kuendelea. Lakini kila mmoja anapaswa kupata angalau saa moja.
Hata kama unafanya biashara ambayo inakuweka kwenye mazingira ya usumbufu wakati wote, bado unapaswa kutenga saa moja kwa siku kwa ajili ya kujifunza na kujiendeleza zaidi. Hivyo wewe saa yako moja ya umakini kwenye siku yako ni ile utakayotenga kwa ajili ya kujifunza. Katika saa hiyo, ondoa kabisa usumbufu wowote unaoweza kuingilia umakini wako.
Ukitenga saa moja kila siku na kuweka umakini wako kwenye jambo moja, na kurudia hivyo kila siku, una nafasi ya kufanya makubwa kwenye maisha yako.
Kila la Kheri Rafiki Yangu.
Rafiki na Kocha wako,
Dr. Makirita Amani,