Moja kati ya kitu ambacho huwa na kiamini sana ni kuwa, kichwa chako kimeumbwa ili kuchukua mambo muhimu ya kuweza kukusadia wewe kufikia mafanikio na sio vinginevyo. Kwa maana hiyo kama una utaratibu wa kubeba mambo mengi kichwani mwako ambayo hayawezi kukusaidia hiyo ni mizigo tena mikubwa unayotakiwa kuitupilia mbali na kubaki kuwa huru.
Watu wengi na mara kwa mara huwa ni watu wa kujibebesha mizigo mingi kichwani mwao isiyowasaidia hata wao. Matokeo yake hukwama na kuanza kulaumu kila hali wanayoijua wao. Lakini, unapochunguza na kuangalia unakuja kugundua watu hao wamejitwisha mizigo mingi sana vichwani mwao isiyo yao, ambayo inayowafanya wawe kama vile vichaa au wasioleweka.
Mambo hayo ambayo siyo msaada kwao au mizigo ambayo wamekuwa wakiishikiria mara kwa mara, ndiyo ambayo imewapelekea  wao katika maisha yao kuishi maisha yasiyofikika kimalengo, maisha magumu, maisha ya majuto na masikitiko kila kukicha. Hii ni hali ambayo wamekuwa nayo pengine bila wao kujua kwamba wanabeba mizigo ambayo haiwahusu.
Je, unajua ni mizigo gani ambayo hutakiwi kuibeba kabisa katika maisha yako ili ufanikiwe?
1.Hofu.
Wengi wengi wamekuwa wakijukuta ni watu wa hofu sana kila kukicha. Hofu hizi mbazo wanazo ndizo ambazo zimekuwa zikiwakwamisha kwa namna moja au nyingine. Wapo watu ambao wao huogopa sana hata kuanza jambo jipya na kulifanikisha. Woga huu, husababishwa na kutokuwa na uhakika na kile kitu kipya wanachota kukifanya.
Sasa kama uko hivi, hapa hakuna suala la kujifariji, huo ni mzigo umejibebesha mwenyewe. Kwa nini nakwambia ni mzigo? Ni kwa sababu maisha yako yote utakuwa unaishi kwa wasiwasi sana kama unaendekeza woga. Na kutokana na hofu hii itakuondolea ujasiri na hutaweza kufanya kitu cha maana kitakachokuwezesha kufikia mipango na malengo yako uliyojiwekea.
Nini kifanyike?
Kwa kuwa umeshagundua umejibebesha mzigo mkubwa wa hofu ndani yako, anza kufanya mambo yatakayokusaidia kukuondolea hofu maishani mwako. Mambo hayo ikiwa pamoja na kujisomea vitabu vizuri vyenye mawazo chanya, kuwa karibu na watu chanya na kutembelea mitandao mizuri kama hii iliyo chini ya AMKA CONSULTANTS.
2. Mawazo hasi.
Hili nalo ni tatizo kubwa ambalo watu wengi wamekuwa wakijibebesha sana pia katika maisha yao. Wengi wetu kutokana  pengine na malezi, mazingira tulimokulia au tabia zetu ziwe za kujitengenezea au kuiga ni watu wa mawazo hasi. Mawazo haya hasi ndiyo yamekuwa yakipelekea harakati  zetu nyingi kukwama siku hadi siku.
Ni rahisi hata wewe mwenyewe kulitambua hili kwa jinsi unavyoishi. Kama wewe ni wa kijicho sana, wivu, tamaa kwa wengine, tambua umebeba mzigo mkubwa ndani yako. Watu wenye mawazo hasi sana kufanikiwa huwa siyo rahisi sana kwao, lakini isitoshe hata afya zao pia zinakuwa sio nzuri. Huu nao ni mzigo kwako unaotakiwa kuutupa ili kufanikiwa.
Kitu gani cha kufanya hapa?
Jifunze mambo mengi chanya ikiwa ni pamoja na kusoma sana vitabu ili kujenga mtazamo chanya zaidi ndani mwako. Ukimudu kufanya hivi kwa muda wa mwezi mmoja, hapo utakuwa umejijengea mawazo mengi sana chanya yatakayokusaidia kuondokana na mawazo hasi.
3. Kuilisha akili yako kila kitu.
Ili uwe mtu wa mafanikio unatakiwa kuilisha au kuipa akili yako vitu vitakavyoweza kuustawisha ubongo wako na kuwa wa ubunifu zaidi. Kwa kadri ubongo wako unavyotengeneza ubunifu ndivyo ambavyo unajikuta hata wewe unakuwa unaongeza uzalishaji mkubwa kwa kile unachokifanya. Hiyo ndiyo kanuni rahisi tu ya ubongo unayotakiwa kuilewa kwa ajili yamafanikio yako.
Sasa wapo watu ambao kila kitu kilichopo kwenye hii duniani wanataka wakiweke kwenyevichwa vyao. Kila habari wanataka iwe ya kwanza kwao kuijua. Haitoshi wao ni watu wa kufatilia kila kitu iwe kwenye televisheni, magazeti na hata umbea ili mradi wasikie. Na mwisho wake hujisahau kujifunza mambo ya kuwasaidia kufanikiwa.  Hata hivyo kumbuka sio na maanisha ni vibaya kujua mambo, lakini uwe na mipaka.
Hiyo yote ni mizigo ambayo wengi wamekuwa wakiibeba sana. Ni vizuri ukajifunza kubeba mizigo mingi lakini ambayo inaendana na kile unachokitaka katika maisha yako. Kinyume cha hapo utakuwa unapoteza muda na kusindikiza wengine kutokana na kuweka mambo mengi yasiyo ya msingi.
Unaweza ukajiuliza mwenyewe tu, je kichwani mwako unamizigo umeibeba isiyo kuhusu au uko huru? Kwa vyovyote vile iwavyo kitu cha msingi kwako, kuwa makini na hofu zinazokutawala, mawazo hasi na kuulisha ubongo wako kila kitu hiyo ni mizigo mikubwa unayojibebesha ambayo haitaweza kukufanakisha katika kitu chochote.
Tunakutakia mafanikio mema, kumbuka TUPO PAMOJA.
Kwa makala nyingine nzuri hakikisha unatembelea DIRA YA MAFANIKIO kila siku kujifunza na kuhamasika.
Ni wako rafiki katika mafanikio,
IMANI NGWANGWALU,
0713 048 035,