Kuna hisia nyingi sana hasi ambazo zinatuzunguka kila siku.

Na hisia hizi ndio zimekuwa zinafanya maisha ya wengi kuwa magumu na ya hovyo.

Alama kubwa ya hisia hasi ni hofu kwenye maisha. Hofu imezuia watu wengi kuishi maisha yenye furaha. Hofu imesababisha baadhi ya watu kuishia kupata magonjwa ya akili. Hofu ni mbaya sana.

utupu

Hisia nyingine kama wivu nazo zinaumiza sana. Wivu unawafanya watu kujiona wa chini, kuona hawawezi na kuishia kuwachukia wengine.

Kuna njia nyingi za kuweza kuondokana na hisia hizi hasi, lakini kuna njia moja ya uhakika sana ambayo itaondoa kabisa hisia hizi.

Akili zetu ni kama debe. Debe linapokuwa na kitu huwa linakuwa limetulia, chukua mfano wa debe lililojaa unga, linatulia vyema.

Ila debe linapokuwa tupu, huwa halitulii, litajaza upepo na upepo huu utakuwa unatoa kelele kali, debe tupu haliachi kuvuma.

Hivyo basi akili yako unapokuwa imejaa inakuwa imetulia. Ila inapokuwa tupu inajazwa upepo na kuanza kuvuma. Upepo na kuvuma ndio hizi hisia hasi.

Unapokuwa huna kitu cha kufikiria na akili yako ipo wazi ndipo unaanza kuzifikiria hofu zako, ndipo unapopata muda w akuchunguza maisha ya wengine na kutengeneza wivu, ndipo unapopata mawazo ya kukata tamaa. Yaani utafanya kila kitu kujaza akili yako. Na mbaya zaidi unaijaza mambo hasi, ambayo ni hatari kwa maisha yako.

SOMA; UKURASA WA 119; Njia Ya Uhakika Ya Kuondokana Na Hofu.

Kuondokana na hofu, wivu na mawazo mengine hasi, hakikisha unaijaza akili yako na mambo ambayo unahitaji kufikiri kweli. Hakikisha unaichoshwa kwa kufanya kazi ambayo inakuhitaji ufikiri, kila muda wa siku yako. na hapa hutapata nafasi ya kufikiria mambo hasi. Ukifika usiku unakuwa umechoka na unataka kulala tu, ukiamka unaendelea na kazi yako inayohitaji kufikiri kwa kina.

Akili yako haiwezi kufikiria mambo mawili kwa wakati mmoja, hivyo unavyoijaza mawazo ya kazi, inasahau mawazo hasi yanayokusumbua.

TAMKO LANGU;

Nimejua njia ya uhakika ya kuondokana na hofu, wivu na mawazo mengine hasi na kuishughulisha akili yangu kwa kufanya kazi ambayo inanihitaji kufikiri sana. Hapa nitaiweka akili yangu bize na haitapata muda wa kufikiria yaliyo hasi. Na hata ninapofika mwisho wa siku, nakuwa nimechoka na nahitaji kulala tu. Kwa njia hii hofu, mashaka na wivu havitakuwa na nafasi tena kwenye akili yangu.

NENO LA LEO.

Anyone that hates on you is always below you, because they’re just jealous of what you have.

Miley Cyrus

Yeyote anayekuchukia mara zote yuko chini yako, ni kwa sababu ana wivu na kile ambacho unacho.

Na kinyume chake pia ni kweli, yeyote unayemchukia upo chini yake, kwa sababu una wivu na kile alichonacho.

Rafiki na Kocha Wako,

Makirita Amani,

makirita@kisimachamaarifa.co.tz

TUPO PAMOJA.