Mpendwa rafiki,
Hakuna mwalimu mzuri anayetufundisha kama maisha. Kuishi tu ni kujifunza, maisa yetu kama kitabu kadiri unavyosoma kurasa nyingi ndivyo unavyokuwa vizuri na kuelewa mambo. Dunia ina kila kitu ambacho tunahitaji shida ni tunavipataje hivyo vitu. Kila mtu anajua ukitaka kufanikiwa unatakiwa kufanya nini na tunawaona hata wenzetu waliofanikiwa sasa kwanini tunashindwa kufanana kama wale waliofanikiwa? Unafikiri shida iko wapi na nini kiini cha yote haya?
Kuna vitu viwili katika maisha yetu ambapo kila binadamu lazima apitie katika maisha yake. Ni vitu vya kawaida sana ila tunapaswa kuvielewa kuwa vitu hivyo viko kwa ajili yetu na siyo kwa ajili ya wengine. tunaalikwa kuhusika na kila kitu kama vile shilingi ilivyokuwa na pande mbili basi hata maisha yako hivyo.
Watu wengi wanaishi falsafa ya ustoa lakini hawajijui kama wao ni wanafalsafa, hata kama wewe siyo mara yako ya kwanza kusoma hapa basi utakua tayari umeshaanza kuishi falsafa na falsafa hiyo nyingine bali ni falsafa ya ustoa. Maisha bila ya kuwa na falsafa yanakuwa hayana msingi na kitu kikosa msingi kinakuwa hakina maana kabisa.
SOMA; Darasa La Wiki; Falsafa Ya Ustoa Na Matumizi Yake Kwenye Zama Tunazoishi.
Rafiki, tunapaswa kuelewa kuwa kuna vitu viwili katika maisha yetu vya kujifunza ambavyo ni kupata na kupoteza. Katika falsafa ya ustoa , wastoa wanaamini kuwa chochote ambacho ni chetu siyo chetu na chochote ambacho siyo chetu siyo chetu. Ukiishi hivyo hata upoteze kitu gani bado utaendelea na maisha yako ya kawaida tu bila kuvurugiwa utulivu wa akili na kushindwa kufanya mambo mengine ya maana.
Kama unapata basi ujue pia kuna kupoteza. Hivyo hicho ulichonacho leo jua kabisa siyo chako na kuna siku utakipoteza hivyo basi unatakiwa kujiandaa kisaikolojia kuwa vyote tulivyonavyo tumeazimwa kwa muda tu na itafikia kipindi utanyang’anywa. Ni ujinga kulalamika na kuona siyo haki yako wewe kunyang’anywa au kupoteza. Kama kwenye biashara unapata faida basi hata kuna siku utapata ni mchezo wa kawaida ambao unapaswa kuuelewa tu.
Sina maana ya kwamba kama tulivyonavyo tunavyo kwa muda hivyo tusijitume wala kujisumbua hapana tujitume na kutafuta zaidi mafanikio lakini tutambue ya kuwa iko siku tutanyang’anywa. Kama unapata jua kabisa na kupoteza ni sehemu ya maisha.
SOMA; Falsafa Bora Itakayokusaidia Kugusa Maisha Ya Watu Wengine.
Hatua ya kuchukua leo, tumia kile ulichonacho vizuri na siku ukikipoteza jua kabisa kupoteza na kupata ni asili ya dunia na wewe kama mwanafalsafa unatakiwa kujijengea hilo kwenye akili yako kuwa hakuna ambacho ni chetu hapa duniani hata siku ukija kupoteza wala hutaumia kama yule mtu ambaye alikuwa hajajiandaa.
Kwahiyo, kama bado huna falsafa ya maisha basi, nakusihii sana jifunze falsafa ya ustoa kwani itakusaidia sana katika zama hizi wakati watu wanataharuki kila siku wewe utakua unaendelea na maisha yako ya kawaida bila usumbufu wowote ule.
Ukawe na siku bora sana ya leo rafiki yangu.
Rafiki na mwalimu wako,
Deogratius Kessy
0717101505/0767101504
deokessy.dk@gmail.com , kessydeo@mtaalamu.net
Unaweza kutembelea tovuti yangu kwa kujifunza zaidi kila siku na kupata huduma mbalimbali kama vile vitabu, kwa kutembelea tovuti hii hapa www.mtaalamu.net/kessydeo .
Asante sana na karibu sana !