Kwa ufuatiliaji mdogo niliofanya kwenye sababu za watu wengi kushindwa kufanikiwa, nilichogundua ni kwamba asilimia kubwa ya vikwazo vya mafanikio ya mtu ni mtu mwenyewe. Yaani sababu kubwa mpaka sasa bado hujapata mafanikio makubwa ni wewe mwenyewe umekuwa unajinyima mafanikio unayostahili. Ni vigumu sana kwako kuamini na kuelewa hili ila ndio ukweli wenyewe, nitajitahidi sana tuwe tunakwenda taratibu kubadili hali hii.

Siku chache zilizopita nilikuwa nakutana na rafiki yangu kwenye hoteli moja kubwa hapa Dar es salaam kwa ajili ya mazungumzo ya kibiashara. Wakati tunaingia kwenye hoteli ile, rafiki yangu alionekana kuwa anajuana na mmoja wa wahudumu ambaye alituhudumia vinywaji, kwani walisalimiana kwa kuitana majina. Tuliendelea na mazungumzo yetu ya biashara, wakati huo yule mhudumu hakuwa mbali sana hivyo alikuwa akisikia kwa mbali. Wakati tunakaribia kumaliza mazungumzo yule mhudumu aliuliza na mimi siwezi kupata hiyo fursa ya biashara? Rafiki yangu akamjibu unaweza, je unataka?

Akasita kidogo kujibu kisa akatoa jibu moja lililonishangaza sana, akasema “kwanza wote hatuwezi kuwa matajiri ndio maana kina Mengi watabaki kuwa kina Mengi na sisi tutabaki kuwa hivi”

Nilimwambia umejibu vizuri sana, nikamuuliza swali moja, “je unaridhika na kazi unayoifanya, kipato unachopata na maisha unayoishi”. Akajibu hapana.

Yaliendelea mazungumzo mengi baada ya hapo, ninachotaka upate hapa ni jinsi gani tumeshajijengea kwenye akili zetu kwamba hatustahili kupata zaidi.

Huyu mwenzetu ni mhudumu wa hoteli kubwa ambaye amefanya kazi hiyo kwa zaidi ya miaka kumi, haimridhishi lakini bado anaamini hastahili kupata zaidi ya hapo. Anaamini kwamba hicho ndio alichopangiwa na hakuna zaidi ya hiko.

Kuna watu wengi sana ambao wana mtazamo kama huu na unawarudisha nyuma kwenye kila hatua wanayofanya. Huenda wewe ni mmoja wa watu hao.

hasi

Unaweza kuwa unahangaika sana kufanya kazi kwa bidii lakini huoni mafanikio. Huenda umejaribu kufanya biashara mbalimbali lakini zote zinaishia kushindwa, umejaribu hata kilimo nako umepata hasara. Unafikiri labda wewe ndio umepangiwa hivyo. Ukweli ni kwamba hicho ndio unachotengeneza kwenye maisha yako. Kama umeshaweka kikomo cha nini unaweza kufanikisha kwenye maisha yako huwezi kupita kikomo hicho hata ungeweka juhudi gani.

Suluhisho pekee ni kuondoa kwanza kikomo ulichoweka kwenye akili yako. Ondoa vizingiti ulivyojijengea au ulivyojengewa na jamii inayokuzunguka. Jua ya kwamba unashathili zaidi ya unachopata sasa, jua ya kwamba unaweza kufanya mambo makubwa kwenye maisha yako. Kwa kubadili hili ndio unaweza kuanza kuona mafanikio makubwa kwenye maisha yako.

Anza kubadili fikra zako ndio uweze kubadili maisha yako. Mawazo yanaleta matendo, matendo yanajenga tabia na tabia inatabiri hatima ya maisha yako.

Ukiwa na mawazo hasi, utafanya matendo hasi ambayo yatakujengea kuwa na tabia ya kushindwa na kukata tamaa na baadae maisha yako yataishia kuwa magumu.

Ukiwa na mawazo chanya, utafanya matendo chanya ambayo yatakujengea tabia ya ubunifu, uvumilivu na kufanikiwa na maisha yako yatakuwa ya mafanikio.

Kabla hujaanza kutafuta mchawi wako nani, anza na mchawi ambaye yuko wazi kabisa ambaye ni wewe mwenyewe.

Nakutakia kila la kheri katika safari ya mafanikio makubwa kwenye maisha yako.

TUKO PAMOJA.

kitabu kava tangazo